Mtayarishaji

Morning Star Radio

Jumapili, Novemba 10, 2013

HOTUBA YA MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, ALIYOITOA BUNGENI KUHUSU JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI, 7 NOVEMBA, 2013, DODOMA



Mheshimiwa Anne Makinda, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi; Mheshimiwa Mizengo Pinda, Waziri Mkuu; Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri; Mheshimiwa Freeman Mbowe, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni; Waheshimiwa Wabunge; Mabibi na Mabwana;

Nakushukuru sana Mheshimiwa Spika kwa kukubali ombi langu na kutenga muda wenu ili niweze kuzungumza na Wabunge wa Bunge lako Tukufu kuhusu masuala muhimu kwa uhai, ustawi na maendeleo ya nchi yetu na watu wake.

Mheshimiwa Spika;

Nimeambiwa kuwa taarifa ilipotolewa kuwa ninaomba kuja kuzungumza na Waheshimiwa Wabunge, kumekuwepo na dhana mbalimbali. Wapo waliodhani kuwa nakuja kuzungumzia mchakato wa kuunda Katiba mpya na hasa matukio ya wiki chache zilizopita. Wapo waliodhani nakuja kuzungumzia “Operesheni Tokomeza”. Tena wapo waliokwenda mbali na kufikiria kuwa nakuja kuwakaripia Waheshimiwa Wabunge waliotoa maoni yao kuelezea kasoro zilizojitokeza katika utekelezaji wa Operesheni hii muhimu. Na wapo pia waliodhani ninakuja kuzungumzia ushiriki wa majeshi yetu ya Tanzania katika Jeshi la Kulinda Amani la Umoja wa Mataifa nchini Kongo.

Mheshimiwa Spika;

Hayo si makusudio yangu. Kinachonileta mbele ya Bunge lako Tukufu ni kuzungumzia Jumuiya ya Afrika Mashariki na mustakabali wa Tanzania katika Jumuiya hiyo. Lakini, kwa sababu ya umuhimu wa masuala hayo niliyoyataja na rai niliyopewa kuwa niyasemee japo kidogo. Nimeona ni vyema nifanye hivyo.

Mheshimiwa Spika;

Kuhusu mchakato wa Katiba mpya, napenda kusema kuwa tumefikia hatua nzuri katika utekelezaji wake. Kama mjuavyo Tume ya Mabadiliko ya Katiba imekamilisha, kwa mafanikio, hatua ya mwanzo ya kusikiliza maoni ya wananchi kuhusu Katiba wanayoitaka. Pia walishatoa Rasimu ya Kwanza ya Katiba na kukamilisha mchakato wa Mabaraza ya Katiba. Kinachosubiriwa kwa hamu na sisi wote, ni Rasimu ya Pili ya Katiba ambayo inatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe 15 Desemba 2013 au kabla ya hapo.

Mheshimiwa Spika;

Kwa upande wa Bunge lako Tukufu, tunategemea kupata mambo mawili kutoka kwenu yatakayowezesha mchakato kutekelezwa vizuri katika hatua zinazofuata. Jambo la kwanza ni kutungwa kwa Sheria ya Kura ya Maoni na pili kufanyika kwa marekebisho ya nyongeza ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kuhusu Bunge Maalum ili kuboresha utekelezaji wake. Baada ya Bunge kukamilisha kazi yake hiyo itafuatia uteuzi wa Wajumbe wa Bunge Maalum ili kazi ya kujadili Rasimu ya Pili ya Katiba ifanyike na kutupatia Rasimu ya Mwisho. Rasimu ambayo ikikubaliwa na wananchi katika Kura ya Maoni itakayofanyika wakati wo wote mwakani, tutakuwa tumepata Katiba Mpya. Hivi sasa katika Serikali tunaendelea kufanya tafakuri na tunachukua hatua za kuwezesha Bunge Maalum na Kura ya Maoni kufanyika kwa mafanikio. Operesheni Tokomeza

Mheshimiwa Spika;

Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge wa Bunge lako Tukufu kuwa sikukasirishwa na maoni yao kuhusu madai ya kuwepo kasoro katika utekelezaji wa Operesheni Tokomeza. Shabaha ya Operesheni hii ni kuokoa maliasili za misitu na wanyamapori dhidi ya uvunaji haramu ambao umefikia kiwango kinachotishia kutoweka kwa raslimali hizo. Kwa kweli hali inatisha. Miti inakwisha na ndovu na faru wanaangamia.

Mheshimiwa Spika;

Wakati, tunapata Uhuru Tanzania ilikuwa na ndovu waliokadiriwa kuwa takribani 350,000. Lakini, kwa sababu ya ujangili uliokithiri katika miaka ya 1970 na 1980 ilipofika mwaka 1989 kulikuwa na ndovu wapatao 55,000 tu. Ilipofikia hali hiyo Serikali ikaanzisha Operesheni Uhai iliyohusisha Jeshi la Ulinzi na kuongozwa na Meja Jenerali John Walden (ambaye sasa ni marehemu) kuendesha mapambano dhidi ya majangili. Kutokana na hatua hiyo na uamuzi wa Shirika linalosimamia biashara ya wanyama walioko kwenye hatari ya kutoweka (CITES) kupiga marufuku biashara ya pembe za ndovu duniani, idadi ya ndovu nchini iliongezeka na kufikia 110,000 mwaka 2009. Tumewaomba Fankfurt Zoological Society ambao ni wabia wetu katika uhifadhi wa wanyama pori kwa miaka mingi wafanye sensa maalum ya ndovu katika Hifadhi ya Selous na kote nchini ili tujue hali halisi ikoje. Kazi hiyo inaendelea hivi sasa.

Mheshimiwa Spika;

Baada ya mwaka 2009 kumezuka wimbi jipya, tena la nguvu kubwa, la kuua ndovu na faru nchini na kwingineko katika Bara la Afrika ambako wanyama hao wapo. Idadi kubwa ya meno ya ndovu yaliyokamatwa na yanaoendelea kukamatwa nchini na kwingineko duniani inathibitisha ukweli huo. Kwa mfano, kati ya mwaka 2010 na Septemba, 2013, hapa nchini, kwa jitihada zetu vipande 3,899 vya pembe za ndovu vyenye uzito wa kilo 11,212 na vipande 22 vya pembe za ndovu zilizochakatwa zenye uzito wa kilo 3,978 vilikamatwa. Aidha, katika kipindi hicho vipande 4,692 vya pembe za ndovu vilivyotokea Tanzania vyenye uzito wa kilo 17,797 vilikamatwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika;

Kama nilivyokwisha sema hapo awali matatizo ya kuuawa kwa wingi kwa ndovu na faru lipo pia katika nchi nyingine Afrika zenye wanyama hao. Nchi za Gabon, Kenya, Afrika ya Kusini, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Uganda, Zimbabwe, Zambia na nyinginezo nazo zinakabiliwa na matatizo kama yetu. Tatizo limekuwa kubwa kiasi cha kuifanya Jumuiya ya Kimataifa kushtuka na kuamua kuingilia kati kwa namna mbili. Kwanza kuunga mkono juhudi za uhifadhi wa ndovu na faru katika nchi zenye wanyama hao. Na, pili, kuchukua hatua thabiti kudhibiti biashara ya meno ya ndovu duniani. Ni ukweli ulio wazi kuwa kama hakutakuwepo na wanunuzi wa meno ya ndovu na faru hakuna ndovu au faru atakayeuawa.

Mheshimiwa Spika;

Kutokana na ukweli ulivyo uamuzi wetu wa kuendesha Operesheni Tokomeza ni sahihi kabisa. Manufaa yaliyopatikana baada ya Operesheni Uhai ya mwaka 1989 yanatupa imani kuwa na safari hii pia tutafanikiwa. Tusipochukua hatua kama hii sasa ni sawa na kuwapa kibali majangili waendelee kumaliza ndovu na faru nchini. Hakika wanyama hao watakwisha. Itakuwa ni aibu kubwa kwetu na historia itatuhukumu vibaya.

Mheshimiwa Spika;

Tumeyasikia maelezo ya Wabunge kuhusu kasoro mbalimbali zilizojitokeza katika utekelezaji wa Operesheni Tokomeza. Nawaahidi kuwa tutayafanyia kazi. Serikali imeahirisha kwa muda Operesheni hii ili kujipa muda wa kurekebisha kasoro hizo na kujipanga upya. Watendaji wasiokuwa waadilifu na wale wasiokuwa waaminifu wataondolewa. Halikadhalika, kasoro za kimfumo nazo zitasahihishwa ili tutakapoanza upya Operesheni itekelezwe kwa mafanikio yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika;

Miongoni mwa mambo yaliyozungumzwa kwa uchungu ni ukamataji wa mifugo iliyokutwa kwenye mapori ya hifadhi za wanyama na vitendo vibaya walivyofanyiwa wenye mifugo na mifugo yenyewe. Narudia kusisitiza kuwa taarifa zote hizo zitafanyiwa kazi na waliohusika watachukuliwa hatua zipasazo. Pamoja na hayo, napenda kuwakumbusha ninyi watunga sheria wetu kuwa sheria ya hifadhi za wanyamapori hairuhusu mifugo kuchungwa katika maeneo ya hifadhi. Naomba tuwakumbushe wananchi tunaowaongoza wajiepushe na kufanya hivyo. Ni uvunjifu wa Sheria za nchi. Naomba pia, wananchi waelimishwe ili wajue kuwa wakifanya hivyo na kukutwa katika maeneo hayo na mifugo yao kuna adhabu iliyotamkwa kwenye sheria. Hivyo tusiwalaumu wala kuwaona maafisa wanyamapori kuwa ni watu wabaya. Wanatekeleza Sheria iliyotungwa na Bunge hili. Pale wanapotenda visivyo tuseme, watawajibishwa ipasavyo.

Jeshi la Umoja wa Mataifa Kongo

Mheshimiwa Spika;

Mapema mwaka huu (2013) Umoja wa Mataifa uliomba nchi yetu ichangie kikosi kimoja cha wanajeshi katika Brigedi Maalum iliyoundwa na Umoja huo kuongeza nguvu ya kudhibiti waasi Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Lengo la msingi ni kuiwezesha nchi hiyo kupata amani ya kudumu ambayo imekosekana kwa muda mrefu kutokana na kuibuka kwa uasi mara kwa mara.

Mheshimiwa Spika;

Tulikubali, kwani hata kabla ya kuombwa na Umoja wa Mataifa tulishakubali maombi kama hayo yaliyotolewa kwenye Mkutano wa Nchi za Maziwa Makuu. Ni miezi saba (tangu Aprili) sasa tangu wanajeshi wetu waende Kongo na wamekuwa wanatekeleza majukumu yao vizuri tena kwa weledi na nidhamu ya hali ya juu. Sifa hiyo kwa wanajeshi wetu imekuwa inatolewa na viongozi wa juu wa Umoja wa Mataifa, viongozi wa juu wa Jeshi la Umoja wa Mataifa Kongo (MONUSCO) na viongozi wa juu wa Serikali ya Kongo.

Mheshimiwa Spika;

Majeshi ya Umoja wa Mataifa hupewa majukumu na mamlaka ya namna mbili. Yapo yanayopewa jukumu la kulinda amani tu. Wanajeshi wake huwa hawapewi majukumu ya kimapigano na hata pale wanaposhambuliwa wanatakiwa kujihami tu. Kwa kawaida majeshi yenye jukumu hili hupelekwa mahali ambapo kumekuwepo na makubaliano ya kuacha mapigano. Wanapelekwa kusaidia kuona Mkataba unatekelezwa ipasavyo. Aina ya pili ni ile ya majeshi yanayopelekwa mahali ambapo hakuna amani hivyo wanapewa jukumu la kuchukua hatua za kufanya amani ipatikane. Majeshi haya hupewa mamlaka ya kutumia nguvu ya kijeshi dhidi ya wanaosababisha amani ikosekane kama ni lazima kufanya hivyo. Maana yake ni kwamba wanayo ruhusa kuingia katika mapigano dhidi ya watu au vikundi vinavyovuruga amani. Tofauti na wenzao wa kundi la kwanza, wanajeshi wa kundi la pili wako kwenye hatari zaidi ya kupoteza maisha au kujeruhiwa kuliko wenzao ingawaje wapo wengi nao wameuawa na kujeruhiwa.

Mheshimiwa Spika;

Wanajeshi wetu wamekwenda Kongo chini ya utaratibu huu wa pili ambao unahusu kuingia kwenye mapigano dhidi ya waasi kama hapana budi kufanya hivyo. Wametekeleza majukumu yao vyema na kwa ujasiri mkubwa na weledi wa hali ya juu. Bahati mbaya tumepoteza vijana wetu watatu shupavu. Daima tutawakumbuka na tutawaenzi ipasavyo mashujaa wetu hawa. Tuzidi kuwaombea kwa Mola awape mapumziko mema. Ameen.

Wakati huo huo, Mheshimiwa Spika, napenda kutumia nafasi hii kumpongeza Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa mafanikio ya kihistoria waliyoyapata hivi majuzi dhidi ya waasi wa M23. Tunamtakia yeye na wananchi wa Kongo kila la heri katika kazi ngumu iliyo mbele yao ya kujenga upya eneo hilo na kujenga mahusiano mapya miongoni mwa watu wa Kongo. Pia nawapongeza sana wanajeshi wa Brigedi Maalum ya Umoja wa Mataifa kwa kazi nzuri waliyoifanya iliyowezesha mafanikio kupatikana. Wanajeshi hao ni kutoka Afrika Kusini, Tanzania na Malawi wanaoongozwa na Brigedia Jenerali James Aloisi Mwakibolwa wa JWTZ.

Jumuiya ya Afrika Mashariki

Mheshimiwa Spika;

Kama nilivyosema awali, haya mambo matatu siyo hasa makusudio yangu nilipoomba kuja kuzungumza na Waheshimiwa Wabunge wetu. Nimeyachomekea tu kwa sababu ya umuhimu wake katika jamii kwa wakati tulio nao. Jambo lililonileta hapa leo ni kuzungumzia hali ilivyo sasa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na nafasi ya Tanzania katika Jumuiya hiyo. Nimeona nifanye hivyo kutokana na maswali mengi ambayo Watanzania wanajiuliza kufuatia matukio ya hivi karibuni ya viongozi wa nchi tatu wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki yaani Uganda, Rwanda na Kenya kukutana bila ya ushiriki wa viongozi wa Tanzania na Burundi. Viongozi wenzangu hao wamefanya mikutano mitatu yaani: tarehe 24-25 Juni, 2013 mjini Entebbe, Uganda; tarehe 28 Agosti, 2013 mjini Mombasa, Kenya; na tarehe 28 Oktoba, 2013 mjini Kigali, Rwanda.

Mheshimiwa Spika;

Naomba kwanza niweke wazi jambo moja, kwamba nchi mbili wanachama au zaidi hazikatazwi kuwa na makubaliano ya ushirikiano katika kufanya mambo mbalimbali. Hata sisi Tanzania tunao ushirikiano wa namna hiyo na nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Lakini, nchi wanachama zinatakiwa kufanya hivyo kwa yale mambo ambayo hayako kwenye shughuli za Jumuiya kwa maana kwamba hayamo katika Mkataba au Itifaki au hakuna uamuzi wa msingi uliofanywa na vikao au taasisi za Jumuiya kuyashughulikia. Pia, tunaweza kufanya hivyo kwa mambo ambayo yalishaamuliwa na Jumuiya yatekelezwe na ruhusa imetolewa kwa nchi yo yote iliyokuwa tayari kutekeleza ama peke yake au kwa kushirikiana na nchi nyingine.

Mheshimiwa Spika;

Kwa mujibu wa matamko ya pamoja (Communique) yaliyotolewa baada ya mikutano hiyo, kuna mambo yapatayo manane ya msingi yaliyoamuliwa kufanywa na nchi hizo kwa lengo la kuendeleza utengamano wa nchi hizo wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Mambo hayo ni haya yafuatayo:

(1)Kujenga reli ya kisasa kutoka Mombasa hadi Kampala, Kigali na Bujumbura. (2)Ujenzi wa Bomba la Mafuta la kutoka Kenya hadi Uganda na Sudani ya Kusini. (3)Kujenga Kiwanda cha kusafisha mafuta nchini Uganda. (4)Kuanzisha Himaya Moja ya Ushuru wa Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na kutekeleza vipengele vyote; (5)Kuharakisha Shirikisho la Afrika Mashariki na kwamba itaundwa Kamati ya kuandaa rasimu ya Katiba ya Shirikisho. (6)Kuharakisha uanzishwaji wa Visa ya pamoja ya Utalii ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (Single East African Community Tourist Visa); (7)Kuandaa utaratibu wa kutumia vitambulisho vya taifa kama hati ya kusafiria katika nchi zao; na (8)Kuongeza uzalishaji na usambazaji wa umeme.

Mheshimiwa Spika;

Ni dhahiri kwamba orodha hiyo imechanganya mambo yale ambayo ni ya Jumuiya na yale yasiyo ya Jumuiya. Kwa mfano, mambo manne kati ya hayo manane hayamo kwenye masharti ya kutokufanyika bila ya kuihusisha au kupata ridhaa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Jambo la kwanza ni uzalishaji na usambazaji wa umeme. Ni kweli kwamba tunao mkakati wa kuwa na akiba ya pamoja ya nguvu ya umeme (East African Power Pool). Hata hivyo, bado jukumu la kuzalisha na kusambaza umeme huo limeachiwa nchi wanachama zenyewe kuamua. Lakini, hivi ndugu zetu hawa wanao muhali kuishirikisha Tanzania katika mpango ambao kimsingi umebuniwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo sote ni wanachama?

Jambo la pili, ni ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta nchini Uganda. Hili si suala la Jumuiya bali la nchi ya Uganda kuamua yenyewe peke yake au kwa kushirikiana na wadau wengine. Rais Yoweri Museveni alituarifu mpango huo na sote tuliupokea kwa furaha kwamba sasa tutapata mafuta karibu na nyumbani. Alitualika kushiriki katika ujenzi wake sijui sasa amebadili mawazo kwamba Tanzania siyo muhimu.

Mheshimiwa Spika;

Jambo la tatu ni ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Kenya hadi Sudani ya Kusini na Uganda. Hili si jambo linalobanwa na masharti ya Jumuiya. Ni juu ya nchi hizi tatu kuamua kufanya ili kuwezesha mafuta yao kufika kwenye masoko. Hata hivyo, nimeambiwa kuwa Jumuiya imeshazungumzia bomba la mafuta kutoka Eldoret hadi Uganda, Rwanda na Burundi kuwa nalo lifike Tanzania kupitia upande wa Kaskazini Magharibi mwa Tanzania. Inaelekea mpango huo sasa haupo maana hatujausikia kutajwa katika ujenzi wa bomba hilo.

Mheshimiwa Spika;

Jambo la nne ni ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Mombasa
– Kampala – Kigali – Bujumbura. Hili nalo hatuna tatizo nalo. Si mradi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ni jambo lililo chini ya mamlaka ya nchi wanachama husika. Hata hivyo, ni vyema kutambua ujenzi wa miundombinu ya reli, barabara na usafiri wa anga na majini kuunganisha nchi za Afrika Mashariki ni miongoni mwa mambo ya kipaumbele cha juu yanayoshughulikiwa na Jumuiya yetu. Jumuiya hutengeneza mikakati ya pamoja na ndiyo maana tuna East African Railway Masterplan, tuna East African Road Network, na tuna Lake Victoria Development Programme kwa ziwa Victoria.

Kwa ajili hiyo, nilitegemea kuwa reli ya kutoka Mombasa hadi Kigali na Juba ingekuwa na tawi linalounganisha reli hiyo na reli ya Tanzania kama ilivyo reli ya Moshi – Voi – Taveta aliyotuachia mkoloni. Tulitegemea hivyo kwa minajili ya kuunganisha soko la Afrika Mashariki ambapo naamini Tanzania ni mdau muhimu. Lakini inaelekea kwa maoni ya wenzetu hivyo sivyo. Mheshimiwa Spika; Lazima nikiri kuwa inashangaza na tunayo kila sababu ya kuuliza kwa nini wenzetu wameamua kufanya hivi. Kumetokea nini toka tukutane pale Arusha Aprili 28, 2013 na Juni 24, 2013 walipokutana kuamua kufanya mambo ya kujenga na kuimarisha utengamano wa Afrika Mashariki kwa kubaguana, Haijawahi kuwa hivi kabla.

Mheshimiwa Spika;

Katika mambo manne yaliyosalia ambayo yaliamuliwa na kuwekewa utaratibu wake wa utekelezaji na Jumuiya ya Afrika Mashariki mawili hatuna maneno nayo. Mambo hayo ni matumizi ya vitambulisho vya taifa kama hati ya kusafiria na Visa ya Pamoja ya Utalii kwani tuliamua kwa pamoja kuwa nchi wanachama zilizokuwa tayari waanze. Lakini, kwa upande wa kuanzishwa kwa Himaya Moja ya Ushuru wa Forodha (Single Customs Territory) na Shirikisho la Afrika Mashariki tunadhani wenzetu wamekiuka uamuzi wetu wa pamoja.

Mheshimiwa Spika;

Katika Mkutano Maalum wa 11 wa Wakuu wa Nchi wanachama uliofanyika tarehe 28 Aprili, 2012 Jijini Arusha, tulipokea na kuridhia mapendekezo ya kuanzisha Himaya Moja ya Ushuru wa Forodha (Single Customs Territory). Kwa mujibu wa mapendekezo hayo kila nchi mwanachama itasimamia shughuli zake za kiforodha na kukusanya mapato yake kama ilivyo sasa. Hata hivyo, kwa bidhaa zinazopitia nchi moja kwenda nchi nyingine mwanachama, ukaguzi na ukusanyaji wa mapato utafanyika katika kituo cha kwanza bidhaa hizo zinapoingilia. Mapato hayo yatawasilishwa kwa nchi husika baada ya kuthibitisha kuwa bidhaa zilivuka mpaka.

Mheshimiwa Spika;

Kutokana na uamuzi huo, Wakuu wa Nchi waliagiza Baraza la Mawaziri kuunda Kikosi Kazi cha kujadiliana na kuandaa utaratibu wa utekelezaji wa mfumo huo. Taarifa ya kikosi kazi inatakiwa kutolewa katika Mkutano wa 15 wa Wakuu wa Nchi utakaofanyika Kampala, Uganda tarehe 30 Novemba, 2013. Iweje leo nchi tatu wanachama ziamue peke yao kuanza kutekeleza? Wanatekeleza nini na kwa nini wafanye hivyo?

Mheshimiwa Spika;

Kuhusu Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki hadithi yake inafanana na hii ya Himaya ya Forodha. Katika Mkutano wa 14 wa Wakuu wa Nchi wanachama uliofanyika tarehe 30 Novemba, 2012, Nairobi, tulipokea taarifa ya hatua iliyofikiwa kuhusu mchakato wa kutaka kuanzishwa kwa Shirikisho. Mkutano huo uliagiza nchi wanachama kujadiliana zaidi kuhusu mpango kazi wa kufikia Shirikisho la Kisiasa na mpango wa kutekeleza mapendekezo mengine yaliyotolewa na Timu ya Wataalamu. Inategemewa kuwa Baraza la Mawaziri litawasilisha mapendekezo ya majadiliano hayo katika Mkutano wa 15 wa Wakuu wa Nchi mwezi Novemba, 2013. Iweje leo wenzetu hawa waamue kuanzisha mchakato wao wa kuharakisha Shirikisho la Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika;

Kwa kweli huwa najiuliza maswali mengi na kukosa majibu kuhusu nini kinachoendelea kufanywa na viongozi wenzangu watatu na kwa nini! Nakosa majibu ya uhakika. Je wenzetu wamekosa imani na Jumuiya ya Afrika Mashariki na je wanataka kuunda yao? Je wanaichukia nchi yetu na hivyo wameamua kutufanyia vitimbi tutoke! Au sijui wanachuki na mimi! Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kuwa hatuna mpango wa kutoka (kama vijana wasemavyo hatoki mtu hapa). Tupo na tutaendelea kuwepo!

Mheshimiwa Spika;

Tanzania haijafanya jambo lo lote baya dhidi ya Jumuiya au nchi yo yote mwanachama. Na ukweli ni kwamba ni mwanachama mvumilivu, mtiifu na mwaminifu kwa Jumuiya. Tunatimiza ipasavyo wajibu wetu kwa Jumuiya na kushiriki kwa ukamilifu katika ujenzi wake na utengamano ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Sabahu ya wenzetu watatu kuamua kufanya mambo yahusuyo Jumuiya yetu peke yao kwa kweli haieleweki.

Mheshimiwa Spika;

Tunasikia eti kuwa baadhi yao walipoulizwa kwa nini wengine hatupo wakasema kuwa wao wametangulia na sisi tutakapokuwa tayari tutajiunga. Yaani wana Umoja wa Waliokuwa Tayari (Coalition of the Willing). Hivi ni nani hayuko tayari (who is not willing?) Haiwezekani watu waitane wenyewe bila ya kutualika halafu wadai kuwa wao ndiyo wako tayari na kujenga dhana kuwa sisi wasiotualika ndiyo ambao hatuko tayari. Madai hayo hayana ukweli. Ni vyema waseme ukweli. Kama walitualika tukakataa ndiyo wanaweza kusema hayo.

Mheshimiwa Spika;

Kumekuwepo na madai kutoka kwa baadhi ya wenzetu, eti kwamba Tanzania haina moyo wala dhamira ya dhati ya kuendeleza utengamano wa Afrika Mashariki. Kwa sababu hiyo inasemekana eti nchi yetu imekuwa kikwazo kwa maendeleo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na kwamba Tanzania tunawachelewesha wengine kupiga hatua za haraka. Wanadai kama siyo hivyo Jumuiya ya Afrika Mashariki ingekuwa mbali kwa maendeleo. Maneno hayo yamekuwa yanarudiwa au kujirudia mara nyingi kiasi cha kuwafanya baadhi ya watu wa Afrika Mashariki na hata kwingineko duniani waamini hivyo.

Mheshimiwa Spika;

Napenda kusema kwa dhati ya moyo wangu kwamba madai hayo hayana ukweli wo wote. Isitoshe hata sababu zinazotolewa kuthibitisha ukweli wake hazina mashiko. Hazifanani na ukweli kuhusu Tanzania na Watanzania walivyo. Tanzania ni muumini wa dhati wa umoja na utengamano wa nchi za Afrika Mashariki na Afrika. Tumethibitisha hivyo kwa vitendo kwa kuunganisha nchi zetu mbili huru yaani Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika na kuwa taifa moja liitwalo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Muungano wa nchi zetu mbili ndio pekee uliodumu kwa muda mrefu kuliko yote Afrika.

Mheshimiwa Spika;

Tanzania ni mwanachama mwaminifu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa maana ya kutekeleza Mkataba ulioanzisha Jumuiya hiyo, kwa Itifaki zake na maamuzi halali ya vikao na taasisi za Jumuiya. Kama lipo jambo ambalo hatujalifanya ilivyotakiwa itakuwa ni kwa sababu za msingi na siyo kwa sababu ya kupuuza Jumuiya. Tunaithamini sana Jumuiya na tumeipa kipaumbele cha juu. Hatuwezi kuhangaika kwa gharama kubwa ya muda wetu, fedha zetu na kutoa mchango wa hali na mali kuianzisha, kujenga na kuifikisha Jumuiya hapa ilipo halafu tuwe ni watu tunaoongoza kutokuipenda na kudhoofisha maendeleo na ustawi wake. Ni maneno ya kushangaza na wala hayaingii akilini. Ama kweli akutukanae hakuchagulii tusi.

Mheshimiwa Spika;

Nionavyo mimi msimamo wetu kuhusu kuharakisha Shirikisho na masuala ya ardhi, ajira, uhamiaji, pengine ndiyo yanayotuletea hisia zisizokuwa sahihi juu yetu. Mimi siamini kama kuna mengine. Hata hivyo, napata taabu kuamini kwamba kutofautiana kwa mawazo katika mambo hayo kutapelekea baadhi ya wenzetu wasipende hata kushirikiana nasi kwa mambo ambayo hayana matatizo na tumekuwa tunashirikiana vizuri.

Mheshimiwa Spika;

Tanzania imekuwa inawasihi wanachama wenzetu kuwa tujenge Jumuiya yetu hatua moja baada ya nyingine kama ilivyo kwenye Mkataba ulioanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki. Hatuna tatizo la kuongeza kasi ya ujenzi wa Jumuiya lakini tusivuke hatua yo yote. Tusiende kasi ya kupindukia. Mkataba unaelekeza tunaanza na Umoja wa Forodha, inafuatia Soko la Pamoja kisha Umoja wa Kifedha na hatimaye Shirikisho la Kisiasa.

Mheshimiwa Spika;

Ni kweli kabisa hatukuunga mkono kuharakisha Shirikisho la Kisasa kabla ya kukamilisha baadhi ya hatua. Na, tulifanya hivyo kwa nia njema ya kutaka Shirikisho lijengwe juu ya msingi imara. Na, msingi huo si mwingine bali utengamano wa kiuchumi kwa maana ya Umoja wa Forodha, Soko la Pamoja na Umoja wa Kifedha zilizojengeka vizuri na kufanya kazi ipasavyo na kunufaisha wanachama wote sawia.

Mheshimiwa Spika;

Lazima tutambue ukweli kuwa kunufaika kiuchumi ndicho kichocheo kikubwa cha nchi kujiunga na kuendelea kuwa mwanachama wa Jumuiya yetu. Kama mambo ya kiuchumi yakipangika vizuri na kila nchi ikanufaika sawia, unajenga msingi imara kwa Shirikisho la Kisiasa kustawi na kudumu. Kama ngazi hizi tatu za awali hazitashughulikiwa vizuri na nchi wanachama zikahisi hazinufaiki ipasavyo, Shirikisho litayumba au kuyumbishwa hivyo kudumu kwake kutakuwa kwa mashaka.

Mheshimiwa Spika;

Tanzania ni kati ya zile nchi zinazotaka ngazi zote za mchakato wa utengamano zitekelezwe moja baada ya nyingine bila kuruka hata moja. Kwa msimamo na mtazamo wetu, Shirikisho iwe ndiyo hatua ya mwisho. Na huo siyo msimamo wangu au wa Serikali peke yake, ndiyo msimamo wa Watanzania walio wengi. Bila ya shaka sote tutakumbuka kuwa mwaka 2006 Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya waliunda Kamati Maalum katika kila nchi kukusanya maoni ya wananchi kuhusu kuharakisha Shirikisho la Afrika Mashariki. Kwa hapa nchini Kamati hiyo iliongozwa na Profesa Samwel Wangwe na katika taarifa yake, Kamati ilieleza kuwa asilimia 74.4 ya Watanzania wanaunga mkono kuwepo kwa Shirikisho lakini ni asilimia 25.4 tu ndiyo waliunga mkono kuharakishwa kwake.

Mheshimiwa Spika;

Takwimu hizi zinaelezea ukweli kuhusu hisia za Watanzania, kuhusu kuwepo kwa Shirikisho na kasi ya utekelezaji wake. Watanzania wengi sana wanaunga mkono kuwepo kwa Shirikisho la Afrika Mashariki lakini wanataka jambo hilo lisifanywe haraka haraka. Wanataka lifanywe kwa umakini mkubwa na tuende hatua kwa hatua kama ilivyoainishwa katika Mkataba uliounda Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika;

Sera na msimamo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inakwenda sambamba na ile ya wananchi wa Tanzania. Ndiyo maana tumeafiki mapendekezo ya Kamati ile ya mwaka 2004 iliyoongozwa na Mheshimiwa Amos Wako wakati ule akiwa Mwanasheria Mkuu wa Kenya. Kamati hiyo iliundwa kupendekeza namna ya kuharakisha utekelezaji wa mchakato wa utengamano wa Afrika Mashariki. Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki umetamka muda wa kutekeleza ngazi ya Umoja wa Forodha lakini uko kimya kuhusu ngazi zilizofuata. Ili kuondoa kasoro hiyo na kwa nia ya kuharakisha Shirikisho Kamati ilipewa jukumu la kutoa maoni na mapendekezo juu ya namna ya kufanya hivyo. Kamati ilifanya kazi nzuri ya kupata maoni na hisia za watu wa makundi mbalimbali katika nchi wanachama kuhusu ujenzi wa Jumuiya na utengamano.

Mheshimiwa Spika;

Kwa upande wa Tanzania kwa mfano, Kamati ya Mheshimiwa Amos Wako ilitambua hisia za Watanzania kuhusu ardhi na ajira na kupendekezwa kuwa masuala hayo yabaki kwenye mamlaka ya nchi wanachama kuamua. Kuhusu mchakato wa utengamano Kamati ilipendekeza kwanza kwamba mchakato wa ujenzi wa Umoja wa Forodha uachwe mpaka ufike ukomo wake wa miaka mitano. Baada ya hapo muda wa kutekelezwa ngazi zinazofuata unaweza kupunguzwa. Kwa mfano walipendekeza kuwa matayarisho ya kuunda Soko la Pamoja yaanze hata kabla ya mchakato wa Umoja wa Forodha kufika mwisho ili mara wakati huo ukifikiwa Soko la Pamoja linaanze. Hivyo hivyo mara baada ya ngazi hiyo kuanza matayarisho ya kuanza ngazi ya Umoja wa Kifedha yanaanza. Ngazi hiyo nayo ikianza matayarisho ya kuunda Shirikisho yanaanza. Kamati pia imetoa mapendekezo ya namna ya kufikia uamuzi kuhusu Shirikisho kwamba wananchi wa nchi wanachama wataamua kwa kura. Tukifuata mapendekezo ya Kamati ya Mheshimiwa Amos Wako na wenzake kama tufanyavyo sasa Tanzania haina matatizo nayo.

Mheshimiwa Spika;

Baada ya kazi kubwa na nzuri iliyofanywa na wana-Afrika Mashariki kuhusu ujenzi wa Jumuiya yao inasikitisha kuona vinafanyika vitendo vinavyoanzisha mivutano kuhusu mambo yaliyokwisha fanyiwa kazi na kuamuliwa. Tunapata taabu zaidi pale watu wanapobagua wenzao na wanapofanya mambo yanayopingana na Mkataba wa Jumuiya na Itifaki zake. Kwa kweli kama mwenendo huu hautabadilika sijui mambo yatakuwaje mbele ya safari.

Mheshimiwa Spika;

Nchi yetu inapenda kuona kuwa tunakuwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyo imara na iliyo endelevu. Jumuiya ambayo inaendeshwa vizuri, mambo yake ni mazuri na nchi zote wanachama na watu wake wananufaika nayo, na hivyo wanaifurahia. Tanzania haina tatizo na kuharakisha mchakato wa utengamano, lakini tunapata taabu kuruka baadhi ya hatua kabla hazijakamilika. Tunawaomba wenzetu kuwa makini katika kila hatua tunayochukua. Bila ya kufanya hivyo, Jumuiya yetu itakuwa imejengeka katika msingi dhaifu hivyo ustawi na uhai wake utakuwa na changamoto nyingi. Hatupendi ya mwaka 1977 yatokee tena.

Mheshimiwa Spika;

Napenda kuwahakikishia kuwa Tanzania itaendelea kushiriki katika shughuli za Jumuiya ya Afrika Mashariki na kuimarisha utengamano wa Afrika Mashariki kwa kuzingatia matakwa ya Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Itifaki zake. Tutafanya kila tuwezalo kuhakikisha kuwa Jumuiya haidhoofiki wala kufa. Na iwapo itadhoofika au kufa kamwe hatutaki Tanzania inyooshewe kidole kuwa chanzo wala kichocheo chake. Ndiyo maana, hatutachoka kuzungumza na wenzetu kuhakikisha kuwa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki inaendelea kustawi.

Tutaendelea kukumbushana umuhimu wa kufanya mambo yanayojenga na kuepuka yale yanayoweza kubomoa. Tutakumbushana umuhimu wa kuheshimu matakwa na masharti ya Mkataba ulioanzisha Jumuiya, Itifaki zake na maamuzi halali ya vikao rasmi na asasi za Jumuiya. Tukifanya hivyo Jumuiya ya Afrika ya Mashariki itadumu, itazidi kustawi na kunufaisha nchi wanachama na watu wake kama yalivyo malengo na madhumuni ya kuundwa kwake.

Mungu Ibariki Afrika Mungu Ibariki Tanzania Idumu Jumuiya ya Afrika Mashariki Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge; Asanteni sana kwa kunisikiliza.

Jumatatu, Novemba 04, 2013

CHAKULA GANI UNAKIPENDA SANA?




Mtu ambaye hula kila kitu asimdharau yule ambaye hawezi kula kila kitu; naye ambaye hula tu mboga za majani asimhukumu anayekula kila kitu, maana Mungu sio kwamba amemkubali bali hajaelewa ni nini Mungu anashauri.

Watu huhitilafiana: mmoja imani yake inamruhusu kula kila kitu; lakini mwingine kwa mujibu wa imani yake hula tu mboga za majani na matunda vyakula vinavyoshauriwa kuvitumia kwa mujibu wa utaratibu wa AFYA..  

Vyakula na mboga za asili ni vile ambavyo vinaota porini na kutumiwa na binadamu. Wengi wetu huviita kama vyakula pori ambavyo ni pamoja na mboga pori, matunda pori ama mizizi pori.

Utafiti uliofanywa umeonyesha kuwa, matumizi ya vyakula asili bado upo Afrika na hapa nchini Tanzania.
 

RASTAFARIAN



Maana alisi ya neno RASTAFARIAN :ni imani ya mtu mweusi au mweupe inayotetea UTU wa MTU MWEUSI.MPIGANIA HAKI YA MTU MWEUSI huitwa RASTAMAN au RASTAWOMAN na kwa WATOTO wao huitwa RASTABABY. 

Imani ya Rasta ilianzishwa zaidi ya miaka 100 iliyopita huku kundi kubwa la waafrika waliokuwa mikononi mwa wakoloni walipoweza kuingia kwenye imani hiyo huku nchi ya JAMAICA ikiwa na wafuasi wengi. Dredy locks ni moja kati ya kitambulisho kikubwa cha Rastafarian,,lakini si kila mwenye dredy locks basi akawa Rastafarian kwani asilimia 25 ya Rastafarian hawana Dredy locks na ndipo tunapoona kwamba kufuga dredy si kuwa na imani ya Rasta bali matendo humpeleka mtu kwenye imani ya Rasta. 

Rastaman hupenda kujiajiri na kufanya shuhguli zake kwa kutumia mikono na si vifaa vya kazi na kati ya kazi za Rasta ni SANAA,, wao hufanya aina zote za sanaa lakini kazi zote hizi Rasta hujiajiri na si kuajiriwa. 

Moja kati ya nguzo za Rastaman ni UPENDO na AMANI,,Rasta hujaribu kutafuta amani popote ipatikanapo, tabia hiyo ya Rast imewafanya Rasta kuheshimiwa popote pale waingiapo lakini baadhi ya jamii huwa tofauti na imani hii. 

 Imani ya Rasta haina chimbuko isipokuwa chimbuko lake ni pale haki ya mtu mweusi ilipo potea na hatimaye jamii kubwa ya watu weusi kutafuta njia ya kutetea utu huo wa mtu mweusi. GABRIEL HAIRE SELASIE aliyekuwa kiongozi wa nchi ya Ethiopia ni moja kati ya watu waliochangia kukuza imani ya Rasta ulimwenguni na ndipo jumuiya ya Rastafariani ilipoamua kumteua kuwa kiongozi wa Rastafarian ulimwenguni. 

Rasta hutumia muda wa mapumziko kwa kusikiliza burudani ya nyimbo walizo zitunga ambazo nyingi ya nyimbo hizo huwa za kuwapa moyo na kuwafariji watu weusi.

Alhamisi, Oktoba 17, 2013

VIJANA HUULIZA


Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kutuma Ujumbe Mfupi?
  • :-) Kunapotumiwa vizuri, kutuma ujumbe mfupi kunaweza kuwa njia nzuri ya kuwasiliana.
  • :-( Kunapotumiwa vibaya kunaweza kuharibu urafiki wako na wengine na kukuharibia sifa.
Makala hii itakueleza mambo unayopaswa kujua kuhusu:
Pia katika makala hii:
 Watu unaotumia ujumbe
Matineja wengi huona kutuma ujumbe mfupi kuwa njia muhimu ya mawasiliano. Kutuma ujumbe mfupi hukusaidia kuwasiliana na watu walio katika orodha yako ya marafiki—⁠isipokuwa iwe wazazi wako hawakuruhusu kufanya hivyo.
“Baba yangu hukasirika mimi na dada yangu tunapoongea na wavulana. Iwapo lazima tuzungumze nao, tunapaswa kufanya hivyo kwa kutumia simu ya kawaida iliyo sebuleni, wengine wakiwapo.”—⁠Lenore.
Unachopaswa kujua: Ukimpa mtu yeyote nambari yako bila kujali, unaweza kujipata matatani.
“Usipokuwa mwangalifu kuhusu ni nani unayempa nambari yako, huenda ukapokea ujumbe au picha mbaya.”—⁠Scott.
“Ukimtumia mtu wa jinsia tofauti ujumbe mara nyingi, unaweza kuanza kuvutiwa naye haraka.”—⁠Steven.
Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Ukichukua hatua fulani za kujilinda, hutapatwa na maumivu mengi.
Simulizi halisi: “Mimi na mvulana fulani tulikuwa marafiki na tulitumiana ujumbe mara nyingi. Nilijiambia kwamba tulikuwa tu marafiki wazuri. Sikudhani kwamba kuna tatizo hadi aliponiambia anavutiwa nami kimahaba. Ninapotafakari yaliyotokea, ninatambua kwamba sikupaswa kutumia wakati mwingi pamoja naye wala kumtumia ujumbe mfupi mara nyingi sana.”—⁠Melinda.
Fikiria hili: Unafikiri urafiki wa Melinda na mvulana huyo utakuwaje baada ya mvulana huyo kumweleza hisia zake?
Badili hadithi hiyo! Melinda angefanyaje mambo kwa njia tofauti ili urafiki wake na mvulana huyo usipite mipaka?
 Mambo unayoandika katika ujumbe
Kwa kuwa ni rahisi sana kutuma ujumbe mfupi—⁠na inafurahisha kupokea ujumbe—⁠huenda mtu akasahau kwamba anaweza kueleweka vibaya.
Unachopaswa kujua: Maneno yaliyoandikwa kupitia ujumbe mfupi yanaweza kueleweka vibaya.
“Unapotuma ujumbe mfupi, mtu hawezi kujua hisia zako hata kama umeweka vibonzo vinavyoonyesha jinsi unavyohisi. Hilo linaweza kufanya mtu akuelewe vibaya.”—⁠Briana.
“Ninajua wasichana fulani ambao wamejiharibia sifa na wanajulikana kuwa wanapenda kuwachezea wengine kimapenzi kwa sababu tu ya ujumbe waliowatumia wavulana hao.”—⁠Laura.
Biblia inasema: “Moyo wa mwadilifu hufikiri kabla ya kujibu.” (Methali 15:28, Biblia Habari Njema) Andiko hilo linatufundisha nini? Soma ujumbe ulioandika kabla ya kuutuma!
 Wakati unaofaa kutuma ujumbe
Kwa busara, unaweza kujiwekea sheria kuhusu kutuma ujumbe mfupi ili kuonyesha una adabu.
Unachopaswa kujua: Usipofuata adabu zinazohusiana na kutuma ujumbe mfupi, huenda ukaonekana kuwa huna heshima na hilo litafanya marafiki wakuepuke badala ya kuvutiwa nawe.
“Ni rahisi kusahau kuwa na adabu unapotuma ujumbe mfupi. Nyakati nyingine, mimi hujipata nikituma ujumbe mfupi huku nikiwa ninazungumza na mtu mwingine au nikiwa mezani ninakula.”—⁠Allison.
“Ni hatari kutuma ujumbe mfupi unapoendesha gari. Ukikengeushwa kwa njia hiyo, unaweza kusababisha aksidenti.”—⁠Anne.
Biblia inasema: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu, . . . wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:1, 7) Kanuni hiyo inatumika pia katika kutuma ujumbe mfupi.
 Madokezo kuhusu kutuma ujumbe mfupi
Watu unaotumia ujumbe
  • ;-) Tii mwongozo wa wazazi wako.—⁠Wakolosai 3:20.
  • ;-) Chagua watu unaowapa nambari yako. Unapokataa kumpa mtu habari za kibinafsi—⁠kutia ndani nambari ya simu yako ya mkononi—⁠unasitawisha stadi ambazo utatumia ukiwa mtu mzima.
  • ;-) Usizoeane isivyofaa na mtu kwa kumtumia ujumbe wa kumchezea kimapenzi. Unapoanza kuvutiwa na mtu kimahaba basi unajitakia maumivu ya moyo na kukatishwa tamaa.
“Nimejijengea jina nzuri pamoja na wazazi wangu kuhusu matumizi ya simu ya mkononi, kwa hiyo wanaamini kwamba nitafanya uamuzi unaofaa kuhusu nambari nitakazoweka katika orodha yangu ya simu.”—⁠Briana.
Mambo unayoandika katika ujumbe
  • ;-) Kabla hujaanza kuandika ujumbe, jiulize, ‘Je, kutuma ujumbe ndio njia inayofaa zaidi ya kuwasiliana katika hali hii?’ Huenda ingefaa upige simu au kusubiri uongee na mtu huyo uso kwa uso.
  • ;-) Usiandike jambo lolote ambalo huwezi kumwambia mtu uso kwa uso. “Ikiwa jambo hilo halipaswi kusemwa kwa sauti, basi halipaswi kuandikwa katika ujumbe mfupi,” anasema Sarah, mwenye umri wa miaka 23.
“Mtu akikutumia picha chafu, waambie wazazi wako. Hilo litakulinda na pia kufanya wazazi wako wakuamini.”—⁠Sirvan.
Wakati unaofaa kutuma ujumbe
  • ;-) Amua kimbele ni wakati gani hutatumia simu yako. Msichana anayeitwa Olivia anasema, “Sibebi simu yangu ya mkononi wakati tunapokula pamoja au ninapojifunza. Mimi huizima wakati wa mikutano ya Kikristo ili nisishawishiwe kuitazama.”
  • ;-) Wajali wengine. (Wafilipi 2:4) Usitume ujumbe mfupi unapozungumza na mtu mwingine.
“Nimejiwekea sheria ya kwamba sitatuma ujumbe ninapokuwa na kikundi cha marafiki wangu isipokuwa iwe ni lazima kufanya hivyo. Pia siwapi watu ambao sina uhusiano wa karibu nambari yangu.”—⁠Janelly.
 Maswali kuhusu kutuma ujumbe
Mfano wa 1
Umekuwa na uhusiano wa karibu na mtu fulani wa jinsia tofauti kwa miezi sita, lakini sasa unagundua kwamba hakufai. Ni ujumbe gani ungefaa kumtumia?
  1. “Uhusiano wetu umekwisha.”
  2. Ningependa kuzungumza nawe. Tunaweza kukutana lini?”
Jibu sahihi: B. Isipokuwa iwe si jambo la hekima kufanya hivyo, ni afadhali kuzungumza na mtu uso kwa uso kuhusu jambo zito kama kukatiza uhusiano.—⁠Luka 6:31.
Mfano wa 2
Unapokea ujumbe mfupi wenye picha chafu ya mwanafunzi mwenzako. Unapaswa kufanya nini?
  1. Kuifuta picha hiyo mara moja.
  2. Kuisambaza picha hiyo kwa marafiki wako wote.
Jibu sahihi: A. Kutuma picha chafu huwashushia heshima wote wanaohusika. Usijihusishe kamwe na jambo hilo!—⁠Waefeso 5:3, 4.
Mfano wa 3
Mnakula pamoja mkiwa familia na unasikia sauti fulani inayokujulisha kwamba umepokea ujumbe mfupi. Unapaswa kufanya nini?
  1. Kusoma ujumbe huo ukitumaini kwamba familia yenu itakuwia radhi.
  2. Kusoma ujumbe huo baada ya mlo.
Jibu sahihi: B. Ujumbe unaweza kungoja. Unapaswa kutanguliza familia.—⁠Wafilipi 1:10.
SOURCE: http://www.jw.org/sw/mafundisho-biblia/familia/matineja/uliza/ninapaswa-kujua-nini-kuhusu-kutuma-ujumbe-mfupi/

Jumanne, Oktoba 15, 2013

SEKTA ZA UCHUMI



Uchumi wa kijadi katika nchi nyingi ulikuwa hasa kilimo cha kujikimu pamoja na biashara ya kubadilishana bishaa kadhaa zenye thamani kubwa. Kwa mfano tangu kale migodi ya Zimbabwe ilichimba dhahabu iliyopelekwa baadaye hadi Asia na dunia ya Mediteranea.
Katika uchumi wa kisasa mara nyinga sekta tatu hutofautishwa:
  • Sekta ya msingi: kutoa na kuzaa malighafi pamoja na mazao katika mazingira asilia. Mifano ni kilimo, uchimbaji wa madini, uvuvi au kuvuna ubao.
  • Sekta ya pili: shughuli za kubadilisha malighafi hizi kuwa bidhaa. Madini ya chuma hubadilishwa kuwa feleji; feleji hutumiwa na viwanda kutengeneza vyuma vya ujenzi, magari, vifaa vya nyumbani. Viwanda vya nguo hutumia pamba kutoka mashambani na kuibadilisha kuwa uzi halafu kitambaa na nguo.
  • Sekta ya tatu: biashara au usambazaji wa bidhaa hizi kwa wateja pamoja na kuwatolea huduma. Mifano ni maduka yanayouza bidhaa zilizotengenezwa viwandani. Mingine ni huduma kama benki, hoteli, sinema na usafiri.
  • Wataalamu wengine hutaja sekta ya nne: shughuli za kusambaza habari na pia utafiti wa teknolojia mpya unaoendelea kuwa muhimu katika nchi zinazoendelea. Wengine huingiza pia elimu (kazi za shule na vyuo) katika sekta hiiy a uchumi.

Sayansi ya Uchumi

Hii ni mkono wa elimu inayochunguza masharti ya uchumi kufaulu au kushindwa.  


Uchumi ni jumla ya shughuli zote za kibinadamu zinazolenga kutosheleza mahitaji ya watu. Ni hasa shughuli za uzalishaji, usambazaji na utumiaji wa bidhaa pamoja na kutolewa kwa huduma kwa njia mbalimbali.
Uchumi mara nyingi hutazamiwa kwenye ngazi za kijiji, eneo, taifa au dunia.

Jumapili, Juni 30, 2013

VIFAA VYA KUTUNZIA KUMBUKUMBKUMBU NJE YA KOMPYUTA VIJULIKANAVYO KAMA REMOVABLE DEVICES.


Kama ilivyo kwa mashine kadhaa na vyombo mbalimbali, kompyuta inaweza kupata hitilafu na hatimaye kupoteza kumbukumbu muhimu sana katika maisha ya kawaida ya jamii. Hivyo panapaswa kuwa na njia mbadala ya kutunza kumbukumbu pindi ikitokea tatizo kama hilo. Kuna vifaa maalum vya kutunzia kumbukumbu ambazo ni muhimu mno. Vifaa hivi huweza kuingizwa katika kompyuta, kuchukua kumbukumbu na kuvitoa kwenda kuvihifadhi mahali ambako ni salama zaidi. Vifaa hivi vinafahamika kama storage devices. Kwa sababu vifaa hivi huweza kutolewa ndani ya system case ya kompyuta hufahamika pia kama removable devices.

Vifaa hivi huingizwa katika Kompyuta kwa kupitia matundu maalum yafahamikayo kama ports na milango maalum ifahamikayo kama drivers. Vyote hivi hujengwa katika system case na huonekana sehemu ya mbele na ama sehemu ya nyuma ya system case.
System case ikiwa na milango na tundu vifahamikavyo kama drivers na port

CD ni nini?

Hiki ni kifaa cha kutunzia kumbukumbu na ambacho kinaonekana kuwa kama kimekuwa mbadala
wa tapes zilizozoeleka kwa muda mrefu katika utunzaji wa muziki na habari mbalimbali. Ni kifaa
ambacho kinatunza kumbukumbu za aina zote; ikiwa na maana text (maneno na picha), sauti na
video. Kifaa hiki kina umbo bapa la mviringo na kina sehemu iliyo kama kioo ambako habari na
data huwekwa. Bila shaka umekwisha kutana na kifaa hiki katika maisha ya kila siku.
 
Picha ya CD

CD ni kifupi cha maneno Compact Disc. Disc hii imetengenezwa kuhifadhi habari na data katika mfumo wa digital, teknolojia mpya ya kuhifadhi kumbukumbu ambayo imeiweka kando teknolojia ya zamani iliyofahamika kama analogue. Kwa mfano mikanda ya muziki na filamu ambayo ilikuwa na mkanda ulioviringishwa katika kifaa kilichoweza kuzunguka na hatimaye kutoa sauti ama kuonesha picha (tazama picha hapa chini) ilikuwa imeundwa kutumia teknolojia ya analogue.      
VHS tapes

CD huingizwa katika kompyuta ili kuwekewa ama kuingiza data na habari katika kompyuta.Kitendo cha kupeleka data na habari kwenye kompyuta hufanywa na kifaa maalum kilicho namlango ambao hufunguka na kufunga na ambao unaweza kubeba CD. Kifaa hiki hufahamika kama CD driver. Mlango huu huwa na taa yenye rangi ya njano-kijani ambayo huwaka pindi CDinapokuwa imewekwa na inafanya kazi ya kusoma data na habari. Kwa kawaida utasikia sauti ya CD kuzunguka katika CD driver. CD driver hufanya kazi ya kuiwezesha kompyuta kuitambua CD na kuifanya ipeleke data au kutoa data. Kazi hii ya kupeleka data au kuifanya kompyuta ipokee habari na data kutoka kwenye CD huitwa reading ama kusoma kwa kiswahili. Kama mtu anakwambia kompyuta inasoma data au habari zilizo katika CD anakuwa anamaanisha kuwa kompyuta hiyo inahamisha data kutoka kwenye CD kwenda katika sehemu ambayo huwezesha data kuonekana kwenye monitor, sehemu ambayo hufahamika kama random access memory

(RAM). Pia kitendo cha kuhamisha data kutoka kwenye kompyuta (yaani hard disk) kwenda kwenye CD hufahamika kama writing ama kuandika. Kitendo cha kuandika habari na data katika CD kutoka mahali zilipohifadhiwa (hard disk) kinawezekana tu kama CD driver ambako CD hiyo huwapo inaweza kuandika habari na data kama itakavyoelezwa hapo baadaye.

Kwa kawaida CD ina uwezo wa kuhifadhi habari ama data zenye ukubwa wa MB 700. Kwa hiyo Kama una habari ama data zenye ukubwa huo na unataka kuzihamishia kwenye kompyuta basi utakuwa unahamisha MB 700 na kama unataka kuzihamisha kutoka hard disk kwenda CD basi utakuwa unahamisha MB 700. Kwa kawaida software nyingi huja zikiwa zimehifadhiwa ndani yaCD na huingizwa katika kompyuta kwa njia ya hizi. Kwa mfano Kama tulivyo sema software mamayaani OS hutakiwa kuingizwa katika hard ware part ya kompyuta ili kuifanya kompyuta ifanyekazi. Software hii huwa ndani ya CD. Kitendo cha kuingiza software ndani ya kompyuta kupitia
CD hujulikana kama installation. Kuna hatua za kufuata katika kufanya kitendo hiki na mara nyingi ni wataalam wa masuala ya kompyuta wanafanya kazi hii. CD pia huhifadhi habari mbalimbali kama muziki, picha za video na za kawaida na data za aina nyingine.

 
Kuna aina kadhaa za CD kulingana na teknolojia ya kuzitengeneza

CD kwa kawaida zimegawanyika katika makundi kadhaa

DVD – aina ya CD yrnyr uwezo mkubewa wa kuhifadhi habari na Data

DVD ni kifupisho cha maneno Digital Versatail Disc. Ni aina ya CD ambao ina uwezo mkubwa wa kuhifadhi data na habari na hakika ni kutokana na uvumbuzi wa kifaa hiki kumeweza kuwa na ubebaji wa data au habari nyingi kwa wakati mmoja. Kifaa hiki kinafanana kabisa kabisa na CD ya kawaida kimuonekano. Tofauti yake na CD ya kawaida ni teknolojia iliyotumika katika utengenezaji. Kwa kawaida CD hutengenezwa ikiwa na sehemu ndogondogo zijulikanazo kama tracks. Tracks hizi huwa katika mpangilio maalum wa mviringo. Kwa sababu CD ni ya Duara, kuna duara nyingi zilizobeba tracks zinazofahamika kama sectors. Data au habari hutunzwa katika kila track ambazo kusanyiko wa tracks huzaa sectors.

Utengenezaji wa CD hutofautiana na ule wa DVD kutokana na mpangilio wa sectors na tracks. Katika DVD kuna tracks nyingi katika sector moja kuliko katika CD ya kawaida. Kwa namna nyingine tunaweza kusema kuwa DVD ina sector nyingi kuliko CD. Kwa namna hii DVD inakuwa na uwezo wa kubeba data nyingi sana kuliko CD. Tuliona kuwa CD ina uwezo wa kubeba data katika uwezo wa kikomo cha MB 700. Hii ni tofauti kwa DVD ambayo ina uwezo wa kubeba data mpaka mara saba zaidi ya ile ya CD. DVD inaweza kubeba data au habari mpaka kufukia MB5000 au GB 5. Ni kwa namna hii ndiyo maana watengenezaji wa filamu na muziki hupenda
kuhifadhi filamu zaidi ya moja (mpaka kufikia 20) katika DVD.

Kama CD pia DVD inaweza kuwa tupu na ukahifadhi data au habari kwa kutumia kompyuta. Hizihuwa zinakuwa katika mfumo wa kuweza kuandikwa. Kuna DVD – R na DVD – RW. DVD – R inasimama badala ya DVD – Recordable ikiwa na maana kuwa unaweza kuhifadhi data kwa kuiandika (writing) mara moja pekee na baada ya hapo inakuwa DVD ya kawaida (yaani ya kusoma tu). DVD – RW inasimama badala ya DVD – Rewritable ikiwa na maana kuwa ina uwezo wa kuhifadhi data au habari zaidi ya mara moja; ikiwa na maana kwamba unaweza kuhifadhi data ukazifuta na kuweka nyingine tena. Hata hivyo kuna ukomo wa kuandika data katika DVD ambapo
inakuwa haina uwezo tena wa kufutwa.

Ili uweze kutumia DVD katika kompyuta inakubidi uwe na DVD river. Hii ni tofauti na DC driver ambayo huwezesha CD kutambulika katika kompyuta. DVD driver imetengenezwa katika tekonlojia ambayo inawezesha kusoma DVD. Kwa kawaida DVD driver huwekwa ktika system case mahali ambako CD driver huwekwa na kuunganisishwa na mothreboard kwa kutumia nyaya zilezile zitumikazo kuunganishia CD driver.

System case ya kompyuta huwa na milango zaidi ya mmoja (inaweza kufikia mitatu) inayowezesha drivers kufungwa na kuunganishwa na motherboard. DVD driver inaweza kuwekwa katika mlango ambao CD driver inatumia. Hata hivyo habari nzuri ni kwamba teknolojia iliyotumika kutengenezea CD driver iitangulia kabla ya ile ya kutengenezea DVD driver, hali inayoifanya DVD driver kuweza kusoma (kutambua) CD na DVDs. Kwa maana hiyo ukiwa na DVD driver katika kompyuta unakuwa na uwezo wa kutumia CD na DVD. DVD driver huwa zimeandikwa DVD ROM au DVD RW katika milango ya kupachika CD au DVD na CD driver huwa zimeandikwa CD ROM au CD RW katika mlango wa kuwekea CD. 

CD & DVD Driver



CD na DVD huweza kutunza data na kumbukumbu kwa muda ambao hutegemea na utunzaji wake. Kwa kawaida CD au DVD huwa na tundu katikati ambalo hutumika kama kishikio

kinachomwezesha mtumiaji kutogusa sehemu ya nyuma ambayo huonekana iking’aa na inayoweza kuonesha taswira mathalani ya uso wa mtu. Sehemu hii ndiyo huwa na data. Kama sehemu hii ikiguswa na uchafu mathalan vumbi na mafuta kutoka mikono ya mtumiaji inaweza kusababisha data kutotumika vyema. Athari ya uchafu katika CD au DVD huonekana mara unapoingiza katika driver ya kompyuta. Haitakuwa inazunguka vyema na itakuwa inakwama kila mara na hii hatimaye hufanya data kutosomeka vyema au kupotea kabisa.

Kwa kawaida CD na DVD huwa zimehfadhiwa katika mifuko laini ya nailoni ambayo huzuia vumbi na uchafu mwingine. Kwa maana hiyo unapotumia CD au DVD inakupasa kuhakikisha kuwa unaiihifadhi vyema katika mifuko ya nailoni na hakikisha kuwa haugusi sehemu zinazong’aa. Kama utahakikisha kuwa unafanya matunzo mazuri basi CD au DVD kitakuwa chombo kizuri cha kuhifadhi data.

Floppy Disk - Kifaa cha kwanza kutunzia na kuhamisha habari au Data katika
Kompyuta

Floppy Disk ni kifaa chenye umbo la penbe nne kama msitatili hivi ambacho kwa muda mrfu kiliyumika kuhifadhi data au kuhamisha data kutoka kompyuta moja kwenda nyingine. Kifaa hiki kina sehemu ndogo laini yenye umbo la mviringo ambayo kwa kawaida huwa imefichwa katika sehemu ngumu ya nyuma na ya mbele. Sehemu ya mbele inaweza kusukumwa mbele na nyuma ili kuwezesha data au habari kuandikwa na kusomwa na kompyuta ndani ya driver ifahamikayo kama floppy driver. Floppy Disk ni tofauti kabisa na Cd au DVD katika ubebaji wa kumbukumbu na data kwani inatumia teknolojia tofauti.







Tofauti na CD au DVD drivers, Floppy driver haina mlango ambao unaweza kufunguka na kufungwa badala yake huwa na tundu dogo la pembe nne ambalo huwezesha floppy disk kuchomekwa kwa kusukuma ndani taratibu. Floppy disk hutolewa ndani ya kompyuta kwa kubonyeza kitufe kidogo kilicho pembeni ya tundu la kuuingizia. Kuna aina mbili za floppy disk drivers, ile ambayo inakuwa kama sehemu ya system case ya kompyuta kama inavyoonekana katika picha A hapo juu na ile ambayo inaweza kuungwa katika kompyuta kwa kutumia waya wa
kuingiza na kutoa data (cable) ifahamikayo kama external floppy driver picha B hapo juu.

Floppy disk inaonekana kutotumika katika miaka ya hivi karibuni kwa sababu teknolojia yake inaonekana kupitwa na wakati. Hii inachangiwa na ukweli kwamba ina uwezo mdogo wa kuhifadi data na kumbukumbu. Ina uwezo wa kubeba na kuhifadhi data na habari zenye ukubwa wa MB 1.35 tu. Hii inaifanya kuweza kubeba habari na data zenye ukubwa mdogo sana ambazo mara nyingi ni maandishi (text files). Kumbuka kuwa kiwango hiki kinazidiwa na DVD kwa zaidi ya mara 5000!

Zip Disk – kifaa cha kutunzia na kubebea kumbukumbu kinachofananishwa
na CD

Kabla ya uzinduzi wa CD palikuwa na kifaa ambacho kiliweza kubeba data na kumbukumbu kwa kiasi kikubwa kama kile cha CD ya kawaida. Kifaa hiki hufahamika kama Zip Disk. Kina umbo sawa na lile la Floppy disk. Ni kifaa ambacho kina uwezo wa kuhifadhi data na kumbukumbu zenye kufikia kiwango cha MB 700. hata hivyo kifaa hiki kinaonekana kutotumika tena na ni wachache sana ambao wanakitumia ni nadra kukuta kompyuta za kisasa zikiwa na Zip Driver, driver ya kuwezesha kompyuta kuitambua Zip Disk.

Hata hivyo system case nyingi za kisasa huwa na CD au DVD driver pamoja na Flopp Driver
pekee.

Memory Stick almaarufu Kama Flash Disk

Hiki ni kifaa ambacho kinatumika sasa katika miaka ya hivi karibuni katika ubebaji na uhfadhi wa data. Ni kifaa kidogo ambacho kinaweza kulingana na kidole gumba cha mtu mzima. Memory stick kinafahamika sana kama Flash Disk kwa watumiaji wengi wa kompyuta na kinaundwa katika maumbo na mtindo mbalimbali. Kinafahamika kama Flash Disk kwa sababu data zake au kumbukumbu zinazohifadhiwa zinaweza kufutwa na kuandikwa kwa muda mfupi na mara nyingi kuliko kifaa kingine kinachoitwa removable storage device. Kifaa hiki kinatofautiana ukubwa wa kuhifadhi data tofauti na vifaaa vingine tulivoviona hapo juu. Memory stick huwa na ukubwa unaoanzia MB 128 mpaka GB zaidi ya 10. Ni kifaa ambacho kinapendwa na watu katika kuhifadhia kumbukumbu kwa sababi ni kidogo kwa umbo na kinaweza kubebwa kwa urahisi hata katika mfuko wa suruali.

Memory stick huwasiliana na kompyuta kupitia matundu maalum yajulikanayo kama (USB ports) Universal serial Bus ports. Haya ni matundu ambayo huwa nyuma na ama mbele ya system case ya kompyuta. Kwa kawaida matundu haya hutumika pia kwa kupachika vifaa kama Mouse, Camera na printers. Memory stick huandikwa ukubwa ilio nao katika sehemu ya nje. Unaweza kukuta memory stick ya kampuni ya Sony ikiwa na MB 512, kwa mfano.

Memory sticks zinatunika sana sasa katika uhamishaji na ukusanyaji wa data na habari na kuhamisha kati ya kompyuta moja na nyingine. Tutaona baadaye madhara ya matumizi ya CD, DVD, Floppy Disk, na Memory stick katika kompyuta.

Memory stick kama vilivyo vifaa vingi vya kielektroniki, imeundwa kwa kutumia muunganiko wa sakiti ndogo ambayo huwa imehifadiwa ndani ya material aina ya plastiki. Unapoishika flash disk unakuwa unaona umbo au material haya ya nje tu ambayo ndani yanakuwa yamehifadhi sakiti inayohifadhi data au habari. Sakiti hii huwa na sehemu iliyotokeza nje ambayo hapa tunaweza kuiita mdomo ambao ndio huingizwa katika tundu la kompyuta (USB port).

Removable devices zina umri wa kuishi!

Kwa kawaida CD, Floppy disk, DVD, na vifaa vinginevyo vya kuhifadhiwa ambavyo vinabuniwa kila kukicha vina muda maalum wa kuhifadhi kumbukumbu. Baada ya muda fulani ambao hutegemea na utunzaji wa kifaa husika kifaa hicho kinakuwa hakina uwezo tena wa kuhifadhi kumbukumbu hizo. Kuna sababu kadhaa ambazo zinafanya vifaa hivi kuishiwa na ama kukosa kabisa uwezo wa kuhifadi tena kumbukumbu. Zifuatazo ni baadhi ya sababu hizo:

Uchafu

Hapa inamaanisha hasa vumbi katika vifaa hivi. Kwa kawaida vifaa kama CD na Floppy Disk huwa na sehemu ambayo huakisi mwanga ambao ndio hufanya kazi ya kutafsiri data na habari. Sehemu hizi kwa kawaida hutakiwa kuwa safi kabisa. Endapo itatokea vumbi na chembechembe zozote za uchafu zikakutana na sehemu hizi basi kumbukumbu zilizohifadhiwa juwakatika hatari ya kupotea. Na mara nyingi dalili ya kutofanya kazi kwa ufanisi ni kukwama-kwama kwa CD au kuchukua muda mrefu kufunguka kwa floppy disk pindi zinapokuwa katika drivers. Hali hii hatimaye husdababisha kompyuta kutosoma kabisa kumbukumbu hizi. Na ndiyo maana watengenezaji wa CD huziweka katika makasha na vifuko maalum ambavyo huzuia vumbi na vitu vingine kuingia katika sehemu ya nyuma ambayo ukiitazama vyema utagundua kuwa ni kama kioo. Pia floppy disk huiifadhi sehemu ya kusoma data ndani ya plastiki ngumu ambayo hufunguka na kubaki wazi pindi inapoingizwa kwenye floppy driver.

Plastiki ama aluminium ambayo huhifadhi sehemu ya kusoma data ambayo hubaki wazi pindi inapoingizwa kwenye kompyuta

Maji ama unyevu

Haya huweza athiri vifaa fivi kwa maana kwamba pindi yanapoingia katika vifaa g