Mtayarishaji

Morning Star Radio

Ijumaa, Machi 30, 2012

Ugonjwa na Sababbu Zake....SURA YA 3


JAMII ya kibinadamu imejiletea yenyewe magonjwa ya aina mbalimbali kwa mazoea yake
mabaya. Hawajajifunza namna ya kuishi kiafya, na ukiukaji wao wa sheria za maumbile
yao, umeleta hali ya mambo ya kusikitisha. Ni mara chache sana watu kama hao wameitaja
sababu halisi ya mateso yao ----- yaani, mwenendo mbaya wa maisha yao. Wamejiendekeza
kwa kutokuwa na kiasi katika kula kwao, na kuufanya uchu wao wa chakula kuwa mungu
wao. Katika mazoea yao yote wameonyesha uzembe katika suala hili la afya na uzima; na
ugonjwa unapowajia, kama matokeo yake, wanajisadikisha wenyewe kwamba ni Mungu
aliyeuleta, ambapo ni mwenendo wao mbaya wa maisha ulioleta matokeo hayo ya hakika.
Wanapozidiwa humwita mganga, na kujisalimisha miili yao mikononi mwake wakitarajia
kuwa atawaponya. Anawapa madawa ambayo hawajui yalivyotengenezwa; na kwa imani
yao ya kijinga wanameza cho chote ambacho mganga huyo anaweza kuchagua na kuwapa.
Kwa njia hiyo wamepewa kunywa sumu zenye nguvu sana, ambazo zinauzuia kabisa mwili
usiweze kufanya juhudi yake yote ya kuyaondoa kutoka mwilini mambo yote yaliyouathiri;
na mgonjwa yule anaharakishwa kuachana na uhai wake.

Mama ambaye amekuwa mgonjwa kidogo tu, na ambaye angeweza kupona kwa kufunga
asile chakula kwa muda mfupi, na kuacha kufanya kazi, akiwa amepumzika kimya, badala
ya kufanya hivyo, anamwita mganga. Na huyo naye, ambaye angekuwa tayari kumpa
maagizo machache yaliyo rahisi, na kumwekea vizuizi katika maakuli yake, na
kumwongoza katika njia sahihi, ama ni mjinga sana kuweza kufanya hivyo, ama ana
wasiwasi sana wa kujipatia malipo.

Anamfanya mgonjwa huyo kuonekana kana kwamba ana ugonjwa mzito sana, naye
humnywesha sumu zake, ambazo, kama yeye mwenyewe angalikuwa mgonjwa,
asingethubutu kuzinywa. Hali ya mgonjwa huyo huzidi kuwa mbaya, na madawa hayo
yenye sumu (drugs) yanatolewa kwake kwa wingi mpaka mwili wake unashindwa kabisa
katika juhudi zake za kuyaondoa mwilini, kisha unasalimu amri kwa mapambano hayo, na
mama huyo hufa. Alipewa madawa mengi hata akafa. Mwili wake ulisumishwa kiasi cha
kutoweza kupona. Aliuawa. Majirani na ndugu zake hushangaa jinsi Mungu anavyofanya
mambo yake ya ajabu kwa kumtwaa mama huyo katikati ya kipindi chake cha manufaa, na
wakati watoto wake wanahitaji sana matunzo yake. Wanamkosea Baba yetu, mwema na
mwenye hekima aliye Mbinguni, hapo wanapomtupia mzigo huu wa misiba ya wanadamu.
Mbingu ilipendezwa kwamba mama huyo aendelee kuishi, na kifo chake cha ghafula
kilimvunjia heshima yake Mungu. Mazoea mabaya ya mama huyo, na kutojali kwake zile
sheria zilizotawala maumbile yake, vilimfanya augue. Na yale madawa ya mtindo wa kisasa
yenye sumu, yaliyoingizwa mwilini mwake, yalikikatisha kipindi cha maisha yake, na
kuliacha lile kundi dogo lisilo na msaada wo wote, lililoshtushwa, na lisilokuwa na mama
kuwa peke yake.

Hayo siyo matokeo ya siku zote yanayoambatana na kunywa madawa haya yaliyotolewa na
mganga. Wagonjwa wanaokunywa madawa hayo yenye sumu huwa wanaonekana kupona.
Kwa wengine wao, wanazo nguvu za akiba za kutosha kwa mwili wao kuweza kuzichota, ili
kuziondoa sumu hizo kutoka mwilini mwao kiasi kwamba wagonjwa hao wakipata muda
fulani wa kupumzika, wanapona. Lakini sifa yo yote isitolewe kwa madawa hayo
waliyokunywa; maana yaliuzuia mwili usiweze kufanya juhudi yake ipasavyo. Sifa zote na
zitolewe kwa uwezo ule ambao mwili unao wa kurejesha afya.

Ijapokuwa mgonjwa huyo anaweza kupona, hata hivyo nguvu zile, ambazo mwili wake
ulizitumia katika juhudi yake ya kuishinda sumu hiyo, zimeathiri afya ya mwili na
kufupisha maisha ya mgonjwa huyo. Kuna wengi ambao hawafi kutokana na kunywa
madawa hayo; lakini kuna wengi sana ambao afya zao zimeharibika hata hawana manufaa
yo yote, hawana tumaini, wamejaa majonzi, nao ni watesekaji wanaosikitisha, wakiwa
mzigo kwao wenyewe na kwa jamii.

Laiti wale wanaokunywa madawa hayo wangekuwa wanateseka peke yao, ubaya huo
usingekuwa mkubwa sana. Wazazi hawatendi dhambi juu yao wenyewe tu wanapokunywa
madawa hayo yenye sumu, bali wanatenda dhambi juu ya watoto wao. Hali chafu ya damu
yao, sumu iliyosambazwa mwilini mwote, afya iliyoharibika, na magonjwa mbalimbali
yatokanayo na madawa hayo yenye sumu, husafirishwa kwa kuingia ndani ya watoto wao,
na kuwaachia kama urithi wao mbaya sana. Hii ni sababu nyingine ya kudhoofika kwa taifa
la wanadamu.

Waganga, kwa kuwapa wagonjwa wao madawa haya yenye sumu, wamechangia sana
kuongeza uchakavu wa taifa la wanadamu kimwili, kiakili, na kimaadili. Ko kote uendako
utaona ulemavu, ugonjwa, na utaahira, hali ambazo, katika hali nyingi, ukizifuatia moja
kwa moja unaweza kukuta kwamba zinatokana na madawa yenye sumu ambayo yalitolewa
kwa mkono wa mganga kama tiba ya baadhi ya magonjwa ya maisha ya mwanadamu. Kwa
njia ya kutisha, ile inayoitwa tiba, imejidhihirisha yenyewe kwa mgonjwa huyo kwa
kumletea mateso makali maishani mwake, ambayo ni mabaya zaidi kuliko ugonjwa ule
ambao kwa huo dawa ile ilinywewa. Wote walio na uwezo wa kawaida wangepaswa
kuelewa mahitaji ya mwili wao wenyewe. Falsafa ya afya ingekuwa mojawapo ya masomo
muhimu kwa watoto wetu. Ni jambo la muhimu kwamba mwili wa kibinadamu ufahamike;
hapo ndipo wanaume na wanawake wenye akili wanaweza kuwa waganga wa kujitibu
wenyewe. Kama watu wangefikiri na kuchunguza sababu yake na kisha matokeo yake, na
kama wangeifuata nuru ile inayowaangazia, basi, wangeifuata njia ile ambayo ingeihifadhi
afya njema, na vifo vingepungua sana. Lakini watu wako tayari sana kubakia katika ujinga
wao usiosameheka, na kujisalimisha miili yao kwa waganga, badala ya kuchukua jukumu lo
lote wao wenyewe.

Mifano kadhaa ya somo hili imeonyeshwa mbele yangu. Wa kwanza ulikuwa ni ule wa
familia ya baba na binti yake. Binti yule alikuwa mgonjwa, na baba yake alihangaika sana
kwa ajili yake, naye akamwita mganga. Yule baba alionyesha wasiwasi mkubwa sana
alipokuwa anamwongoza [mganga yule] katika chumba kile cha mgonjwa. Mganga
akampima mgonjwa yule, wala hakusema mengi. Wote wawili waliondoka katika chumba
cha mgonjwa yule. Baba yule akamjulisha mganga kwamba alikuwa amemzika mama yake
[binti yule], mwanawe, na binti, na ya kwamba binti yule ndiye peke yake aliyebaki kwake
katika familia yao. Kwa wasiwasi akamwuliza yule mganga endapo alifikiri suala la binti
yake lilikuwa halina matumaini yo yote.

Ndipo mganga yule alipomhoji kuhusu aina ya ugonjwa na muda waliochukua wale
waliokufa. Kwa sauti ya kuomboleza baba akasimulia habari ya kuhuzunisha kuhusu
ugonjwa wa wapendwa wake. "Mwanangu alishambuliwa kwanza na homa. Nikamwita
mganga. Alisema angempa dawa ambayo ingeikomesha homa ile mara moja. Alimpa dawa
yenye nguvu, walakini alisikitishwa na matokeo yake. Homa ikapungua, lakini mwanangu
akaendelea kuwa mgonjwa mahututi. Dawa ile ile tena alipewa, bila kuleta mabadiliko yo
yote mema. Mganga yule ndipo alipotumia dawa zenye nguvu zaidi, lakini mwanangu
hakupata nafuu yo yote. Homa ikamwacha, lakini hakupata nguvu tena. Alinyong'onyea
upesi na kufa.

"Kifo cha mwanangu, cha ghafula na kisichotazamiwa, kilituletea sisi sote majonzi
makubwa, hasa mama yake. Kule kukesha kwake na wasiwasi wake wakati wa ugonjwa
wake [mwanangu], na majonzi yake kutokana na kifo chake cha ghafula, vilikuwa
vimezilemea mno neva zake, naye akawa amenyong'onyea kabisa kwa upesi sana. Mimi
sikujisikia kuridhika na njia ile aliyoitumia mganga yule. Imani yangu katika utaalam wake
ilikuwa imetikiswa, nami sikuweza kumwajiri mara ya pili. Nikamwita mwingine kuja
kumtibu mke wangu aliyekuwa anateseka. Mganga huyu wa pili alimpa afyuni [opium] kwa
wingi sana ambayo alisema ingeweza kumpunguzia maumivu yake, kutuliza neva zake, na
kumpumzisha, jambo ambalo alikuwa analihitaji sana. Afyuni ile ikampumbaza. Akalala
usingizi, na hakuna kitu kilichoweza kumwamsha kutoka katika usingizi huo wa kifo.
Mapigo ya mishipa yake na moyo wakati mwingine yalipiga kwa nguvu, na halafu
yakapungua na kuwa dhaifu zaidi na zaidi mpaka alipoacha kupumua. Hivyo ndivyo
alivyokufa, bila hata mara moja kuitazama na kuitambua familia yake. Kifo hiki cha pili
kilikuwa kichungu zaidi ya vile tulivyoweza kustahimili. Wote tulihuzunika sana; lakini
mimi niliumia vibaya sana, wala sikuweza kufarijiwa.

"Binti yangu ikawa zamu yake kuteseka. Majonzi, kiherehere, na kukesha vilikuwa
vimezimaliza nguvu zake za kustahimili, na nguvu zake zikaisha, naye akalazwa juu ya
kitanda chake cha mateso. Sasa nilikuwa nimepoteza imani yangu kwa waganga hao wote
wawili niliowaajiri. Mganga mwingine akapendekezwa kwangu kuwa amefanikiwa
kuwatibu wagonjwa; na ijapokuwa alikuwa anakaa mbali, niliazimu kupata huduma zake.
"Mganga huyo wa tatu alidai kwamba anaujua ugonjwa wa binti yangu. Akasema alikuwa
amedhoofika sana, mishipa yake ya fahamu ilikuwa imeharibika, na ya kwamba alikuwa na
homa, ambayo ingeweza kudhibitiwa, lakini ingemchukua muda mwingi kumtoa katika hali
yake ya sasa ya udhaifu. Alionyesha imani kamili katika uwezo wake wa kumrejesha katika
hali yake ya kawaida. Akampa madawa yenye nguvu ili kuivunjilia mbali homa ile. Hilo
likawa limekwisha. Lakini homa ilipomwacha, mgonjwa yule akawa na dalili za kuogofya,
nazo zikawa ngumu zaidi. Dalili hizo zilipobadilika, dawa nazo zikabadilishwa kulingana
na ugonjwa. Wakati anatumia dawa mpya alionekana kwa wakati fulani kama anapata
nafuu. Jambo hilo lilitutia matumaini kwamba atapona, lakini alipoendelea kuwa na hali
mbaya zaidi jambo hilo lilikufanya kukata tamaa kwetu kuwe kuchungu sana.

"Dawa ya mwisho aliyotumia mganga huyo ni aina ya dawa ya kuharisha iitwayo kalamelo
[calomel]. Kwa muda fulani alionekana kuning'inia kati ya uzima na kifo. Akaanza
kufurukuta kana kwamba ana kifafa. Mahangaiko hayo ya kufurukuta yalipokoma,
tulizinduka na kuuona ukweli kwamba akili zake zilikuwa zimedhoofika sana. Pole pole
akaanza kupata nafuu, japokuwa alikuwa bado anateseka sana. Mikono na miguu yake
ilikuwa imepooza kama matokeo ya sumu zile zenye nguvu alizokunywa. Aliendelea kuwa
hai kwa miaka michache, akiwa mtesekaji asiyejiweza na mwenye kutia huruma, naye
alikufa akiwa na maumivu makali sana."

Baada ya kusimulia kwa huzuni baba huyo akamtazama mganga yule kwa mtazamo wa
kumsihi, na kumwomba sana apate kumwokoa mtoto wake wa pekee aliyebaki. Mganga
yule alionekana amehuzunika na mwenye mashaka, lakini hakutoa dawa zo zote.
Alisimama na kuondoka, akisema kwamba angerudi siku iliyofuata.

Tamasha nyingine ikaletwa mbele yangu. Nililetwa mbele ya mwanamke mmoja, mwenye
umri wa karibu miaka thelathini hivi. Mganga alikuwa amesimama kando yake, na kutoa
taarifa yake kwamba mishipa yake ya fahamu [mgonjwa yule] ilikuwa imeharibika,
kwamba damu yake ilikuwa chafu na mzunguko wake mwilini ulikuwa wa pole pole, na ya
kwamba tumbo lake la chakula lilikuwa katika hali ya ubaridi na halifanyi kazi. Akasema
angempa madawa yenye nguvu ambayo yangeiboresha hali yake. Akampa dawa fulani ya
unga kutoka kwenye chupa ndogo iliyoandikwa 'Nux Vomica.' Nikaangalia kuona matokeo
yake yatakuwaje juu ya mgonjwa huyo. Ilionekana kuwa na matokeo mazuri. Hali yake
ilionekana njema zaidi. Akawa amechangamka, na hata kuonekana mkunjufu na mwenye
uwezo wa kufanya vitu fulani.

Kisha mawazo yangu yakaelekezwa kwa mgonjwa mwingine zaidi. Nikaingizwa katika
chumba cha mgonjwa mwanaume kijana aliyekuwa na homa kali sana. Mganga alikuwa
anasimama kando ya kitanda cha mtesekaji huyo akiwa na kifungu cha dawa kutoka katika
chupa ndogo iliyoandikwa 'calomel' [kalamelo]. Akampa kemikali hii yenye sumu, na
badiliko likaonekana kuwa linatokea, ila si kwa hali iliyo nzuri zaidi.

Kisha nikaonyeshwa mgonjwa mwingine. Alikuwa mwanamke, ambaye alionekana kama
anapata mateso mengi sana. Mganga alisimama kando ya kitanda cha mgonjwa huyo, naye
alikuwa anamnywesha dawa aliyoichukua kutoka katika chupa ndogo iliyoandikwa juu
yake 'Opium' [afyuni]. Mwanzoni dawa hii ilionekana kuleta madhara katika ubongo.
Akawa anazungumza kiajabu, lakini hatimaye alinyamaza, na kulala usingizi.

Kisha mawazo yangu yakaelekezwa kwa mgonjwa yule wa kwanza, yaani, baba yule
aliyekuwa amempoteza mkewe na watoto wake wawili. Mganga yule alikuwa katika
chumba cha mgonjwa, akiwa amesimama karibu na kitanda cha binti yule aliyekuwa
anaumwa sana. Akaondoka tena pasipo kumpa dawa yo yote. Baba yule, akiwa peke yake
mbele ya mganga yule, alionekana kuguswa sana, naye akauliza bila kuwa na subira, "Je!
unakusudia kutofanya kitu cho chote? Je, utamwacha afe binti yangu huyu aliyebaki peke
yake?

Mganga akajibu: "Nimesikiliza historia ya kusikitisha ya kifo cha mke wako uliyempenda
sana na kile cha watoto wako wawili, nami nimejifunza kutoka kinywani mwako
mwenyewe kwamba wote watatu walikufa wakiwa wanahudumiwa na waganga, na wakati
walipokuwa wakinywa dawa zile zilizoamriwa na kutolewa kwa mikono yao. Dawa
haijawaokoa wapendwa wako; na mimi kama mganga, naamini kwa dhati kwamba hakuna
hata mmoja wao ambaye angehitaji, ama angestahili, kufa. Wangeweza kupona kama
wasingalikuwa wamenyweshwa kwa wingi madawa hayo ya sumu kiasi kwamba mwili wao
ulidhoofika kwa kuhudumiwa vibaya, na hatimaye ukaangamia." Kwa uthabiti akamweleza
baba huyo aliyekuwa amefadhaika: "Siwezi kumpa dawa binti yako. Nitahitaji tu kuusaidia
mwili wake katika juhudi zake, kwa kuondoa kila kizuizi, na kisha kuyaacha maumbile
yenyewe kurejesha nguvu zake zilizopotea mwilini." Akaweka mkononi mwa baba huyo
maagizo machache ambayo alimwagiza kuyafuata kwa karibu sana: "Mfanye mgonjwa
asiwe na wasiwasi wo wote, na kumwepusha na mvuto wo wote unaoweza kumfanya
ahuzunike. Wanaomtunza wawe wachangamfu na wenye matumaini. Apewe chakula cha
kawaida, na maji safi ya kunywa kwa wingi. Aoge mara kwa mara akitumia maji safi, na
tiba hii ifuatiwe na kumsugua mwili kwa pole pole. Acha mwanga na hewa safi viingie kwa
wingi ndani ya chumba chake. Anatakiwa kupumzika kwa utulivu na bila ya kusumbuliwa."
Baba huyo kwa pole pole akasoma maagizo hayo ya mganga, akishangaa kwa maelekezo
machache mno yaliyo rahisi yaliyokuwamo ndani yake, naye akaonekana kuwa na mashaka
kwamba jambo jema lo lote linaweza kutokea kutokana na njia hizo rahisi.

Mganga akamwambia: "Umekuwa na imani ya kutosha katika utaalam wangu kiasi cha
kuweka maisha ya binti yako mikononi mwangu. Usiiondoe imani yako hiyo.
Nitamtembelea binti yako kila siku, na kukuelekeza namna utakavyomshughulikia. Fuata
maagizo yangu kwa imani, nami natumaini kumkabidhi mikononi mwako katika muda wa
majuma machache akiwa katika hali nzuri zaidi ya afya, kama sio kupona kabisa."
Baba huyo alionekana amehuzunika na mwenye mashaka, ila akatii maamuzi ya mganga
yule. Alikuwa na hofu kwamba binti yake lazima atakufa tu, kama hakupewa dawa yo yote
ile.

Mgonjwa yule wa pili akaletwa tena mbele yangu. Mgonjwa yule alionekana anapata nafuu
zaidi baada ya kunywa dawa ile ya 'Nux Vomica.' Alikuwa ameketi, akikunja shali yake na
kujifunika mwili wake, akilalamika kwamba anasikia baridi. Hewa katika chumba hicho
ilikuwa chafu. Ilikuwa ya joto sana, na kupoteza nguvu yake. Karibu kila kipenyo ambacho
kingeweza kuingiza hewa safi kilikuwa kimezibwa, kumhifadhi mgonjwa huyo asijisikie
baridi sana, ambayo alikuwa anaisikia hasa upande ule wa nyuma wa shingo yake na
kutelemka katika uti wake wa mgongo. Mlango ulipoachwa wazi, alionekana anahangaika
na kuwa na wasiwasi, na kusihi kuwa ufungwe, maana alikuwa na baridi. Hakuweza
kustahimili upepo kidogo uliokuwa unaingia kupitia mlangoni au madirishani. Mwanaume
mmoja mwenye akili alisimama akimwangalia kwa huzuni, na kuwaambia wale
waliokuwapo: "Haya ndiyo matokeo ya pili ya dawa hii ya 'Nux Vomica.' Matokeo hayo
yanasikika kwenye mishipa ya fahamu, na kuathiri mfumo wote wa mishipa ya fahamu.
Kwa kipindi fulani kutakuwa na msongo utakaozilemea neva. Lakini nguvu ya dawa hii
itakapokwisha, kutakuwa na ubaridi na unyong'onyevu. Kwa kiwango kile kile
inavyochochea na kutia nguvu mwilini ndivyo matokeo yake yatakayofuata yatakavyokuwa
ya kudhoofisha na kupoozesha."

Mgonjwa wa tatu alipitishwa mbele yangu tena. Alikuwa ni yule mwanaume kijana
aliyenyweshwa dawa ya kalamelo (calomel). Aliteseka sana. Midomo yake iligeuka rangi
na kuwa myeusi na kuvimba. Fizi zake zilivimba na kuwa nyekundu. Ulimi wake ulikuwa
mnene, umevimba, na mate mengi sana yalikuwa yakimtoka kinywani mwake.
Mwungwana yule mwenye akili aliyetajwa huko nyuma akamtazama kwa huzuni mgonjwa
yule aliyekuwa anateseka, na kusema: "Haya ndiyo matokeo ya michanganyo ya zebaki
(mercurial preparations). Kijana huyu alikuwa amebakiwa na nguvu ya neva ya kutosha
kuweza kuanza mapambano na mgeni huyu asiyetakiwa, yaani, dawa hii yenye sumu, na
kujaribu kuiondoa mwilini. Wengi hawana nguvu ya akiba iliyobaki ya kutosha kufanya
kazi hiyo; na maumbile yanashindwa kabisa, na kuacha juhudi zake, na mhanga huyo
anakufa."

Mgonjwa wa nne, yule mtu aliyepewa afyuni (opium), aliletwa tena mbele yangu.
Akaamka kutoka usingizini akiwa amepooza sana. Mawazo yake yalikuwa
yamesambaratika. Alikuwa hana uvumilivu na mwenye harara, akiwakosoa rafiki zake bora
sana, na kufikiri ya kwamba walikuwa hawajitahidi kumpunguzia maumivu yake.
Akarukwa na akili na kuanza kupayukapayuka kama mwenda wazimu. Yule mwungwana
aliyetajwa huko nyuma akamtazama kwa huzuni mtesekaji huyo, na kuwaambia wale
waliokuwapo: "Haya ndiyo matokeo ya pili ya kunywa afyuni."

Mganga wake akaitwa. Akampa kipimo kikubwa zaidi cha afyuni, ambacho kilinyamazisha
upayukaji wake, walakini kikamfanya kuwa msemaji sana na mchangamfu. Alikuwa na
amani na wote waliomzunguka, na kuonyesha upendo mwingi kwa wale waliomfahamu,
pamoja na ndugu zake. Mara hiyo akaanza kusikia usingizi mzito ukimjia, naye akalala
kama mtu aliyeduwaa. Mwungwana aliyetajwa hapo juu kwa huzuni kuu akasema: "Hali
yake ya sasa si bora kuliko aliporukwa na akili na kupayukapayuka. Kwa hakika hali yake
sasa ni mbaya zaidi. Dawa hii yenye sumu ya afyuni inampa mgonjwa nafuu ya maumivu
kwa muda tu, lakini haiondoi sababu iliyoleta maumivu hayo. Inaupumbaza tu ubongo, na
kuufanya usiwe na uwezo wa kupokea habari kutoka kwenye mishipa ya fahamu. Ubongo
unapokuwa katika hali hiyo ya kutotambua cho chote, fahamu zile za kusikia, kuonja, na
kuona zinaathirika. Nguvu ya afyuni inapokwisha mwilini, na ubongo unapozinduka kutoka
katika hali yake ya kupooza, mishipa ya fahamu ambayo ilikuwa imekatiwa mawasiliano
yao na ubongo, sasa inapiga kelele kubwa sana kuliko ilivyopata kufanya, ikitoa taarifa ya
maumivu yalivyo mwilini, kwa sababu ya ukatili wa ziada ambao mwili umestahimili
katika kuipokea sumu hiyo. Kila ongezeko la dawa hiyo yenye sumu alilopewa mgonjwa
huyo, kama ni afyuni au dawa nyingine yo yote, litamfanya mgonjwa huyo kuwa na
matatizo mengi zaidi, na kufanya tumaini la kupona kwake liwe la kukatisha tamaa.

Madawa yatolewayo yanayopumbaza, haidhuru yawe madawa ya aina gani, huharibu
mfumo mzima wa neva mwilini. Baa, lililo rahisi mwanzoni, ambalo maumbile yenyewe
yaliamka na kuanza kulishinda, na ambalo yangelishinda kama yangaliachiwa kazi hiyo
yenyewe, sasa limekuwa baya mara kumi zaidi kwa kutumia madawa haya yenye sumu
mwilini. Matokeo ya sumu hizo ni ugonjwa unaoangamiza uletwao nazo, na kuzilazimisha
nguvu zile za akiba zilizobaki mwilini kufanya kazi ya ajabu mno ya kupigana na kuishinda
dawa hiyo yenye sumu iliyoingia mwilini kama mgeni asiyetakiwa."





Nilipelekwa katika chumba kile cha mgonjwa yule wa kwanza, yule baba na binti yake.
Binti yule alikuwa ameketi kando ya baba yake, akiwa amechangamka na mwenye furaha,
na mng'aro wa afya ukiangaza usoni pake. Baba alikuwa anamwangalia akiwa ameridhika
na kufurahi, uso wake ukionyesha shukrani ya moyoni mwake, kwamba mtoto wake wa
pekee alikuwa ameachwa hai kwa ajili yake. Mganga wake akaingia, na baada ya
kuzungumza na baba na mtoto kwa muda mfupi, akasimama na kuondoka. Akamwambia
baba yake hivi: "Mimi nakukabidhi binti yako akiwa amerejeshewa afya yake. Sikumpa
dawa yo yote, ili nimwache akiwa na afya kamili ya mwili wake. Dawa kamwe isingeweza
kufanya hivyo. Dawa inaharibu mashine nyororo ya mwili, na kuua, walakini haiponyi
kamwe. Mwili peke yake unazo nguvu za kurejesha afya ya mwili. Huo peke yake unaweza
kuzijenga upya nguvu za mwili zilizotumika, na kukarabati majeraha uliyopata kwa
kutozijali sheria zake zisizobadilika."

Kisha akamwuliza yule baba kama alikuwa ameridhika na aina ya matibabu yake aliyotoa.
Baba yule mwenye furaha alitoa shukrani zake za dhati na kuridhika kabisa, akisema,
"Nimepata fundisho ambalo sitalisahau kamwe. Lilikuwa chungu, lakini lina thamani
isiyopimika. Sasa nimesadiki kwamba mke wangu na watoto wale wasingekuwa na haja yo
yote ya kufa. Maisha yao yalitolewa mhanga wakiwa mikononi mwa waganga wale
waliowapa madawa yao yenye sumu."

Kisha nikaonyeshwa mgonjwa yule wa pili, ----- aliyepewa kunywa dawa ile ya 'Nux
Vomica.' Alikuwa ameshikiliwa na wahudumu wawili kutoka kwenye kiti chake kwenda
kwenye kitanda chake. Alikuwa karibu amepoteza nguvu ya viungo vyake. Mishipa ya
fahamu ya uti wake wa mgongo ilikuwa nusu imepooza, na miguu yake ilikuwa imepoteza
nguvu yake ya kuutegemeza uzito wa mwili wake. Alikohoa kwa shida, na kupumua kwa
shida. Akalazwa juu ya kitanda, na mara hiyo akawa amepoteza uwezo wake wa kusikia na
kuona; na baada ya kukaa hivyo kwa muda mfupi, akafa. Yule mwungwana aliyetajwa huko
nyuma akauangalia kwa huzuni mwili ule uliolala chini ukiwa hauna uhai, na kuwaambia
waliokuwapo pale: "Shuhudieni matokeo ya muda mrefu ya dawa hii ya 'Nux Vomica'
katika mwili wa mwanadamu. Mwanzo wake, nguvu ya mishipa ya fahamu ilichochewa
kufanya mambo ya ajabu kutokana na dawa hiyo yenye sumu. Msisimko huo wa ziada
ulifuatiwa na unyong'onyevu, na matokeo ya mwisho ni kupooza kwa neva. Dawa hii yenye
sumu haina matokeo yanayofanana kwa wote. Wengine, walio na miili ya afya yenye
nguvu; hupona kutokana na madhara ambayo dawa hii inauathiri mwili wao vibaya;
ambapo wengine, ambao maisha yao yanalegalega, ambao wana miili dhaifu kiafya,
hawaponi kamwe kwa kunywa hata kipimo kimoja tu cha dawa hii. Daima matokeo yake
huelekea kwenye kifo. Hali ya mwili ilivyo, wakati wa kuingiza sumu hizo ndani yake,
huamua uhai wa mgonjwa utakavyokuwa. 'Nux Vomica' inaweza kufanya afya ya mtu
ipungue, apooze, ama iharibike milele, bali kamwe haiponyi ugonjwa."

Mgonjwa wa tatu ----- mwanaume yule kijana aliyepewa sumu ya kalamelo -----
alipitishwa tena mbele yangu. Alikuwa mtesekaji mwenye kutia huruma. Miguu yake
ilikuwa imepooza, naye alikuwa ameharibika sana. Alisema kwamba mateso yake yalikuwa
hayaelezeki, na ya kwamba kwake maisha yalikuwa mzigo mzito sana. Yule mwungwana
ambaye nimerudia tena na tena kumtaja akamtazama kwa masikitiko na huruma mtesekaji
huyo, na kusema: "Hayo ndiyo matokeo ya kalamelo. Sumu hiyo inaendelea kuutesa mwili
kadiri chembe moja ya sumu hiyo inavyobaki humo. Inaendelea kufanya kazi yake, bila
kupoteza nguvu zake kwa kukaa sana katika mwili ulio hai. Inavifanya viungo vivimbe, na
mara nyingi kupeleka uozo ndani ya mifupa. Mara kwa mara inajidhihirisha yenyewe katika
tezi zilizovimba, vidonda, kansa, miaka mingi baadaye baada ya kuingizwa mwilini."
Mgonjwa wa nne aliletwa tena mbele yangu, ----- mgonjwa yule aliyepewa afyuni. Uso
wake ulikuwa rangi ya manjano nyeupe, na macho yake yalikuwa hayatulii na yanang'aa
kama kioo. Mikono yake ilitetemeka kana kwamba imepooza, naye alikuwa na wasiwasi
sana akidhani ya kwamba wote waliokuwapo pale walikula njama dhidi yake. Ubongo wake
ulikuwa umeharibika kabisa, naye alikuwa anapayukapayuka kwa njia ya kutia huruma.
Mganga akaitwa, naye hakuonekana kushtuka na maono hayo ya kutisha. Akamnywesha
mgonjwa wake kifungu kingine chenye nguvu zaidi cha afyuni, ambacho alisema
kitamweka sawa. Kupayukapayuka kwake hakukukoma mpaka hapo alipokuwa amelewa
kabisa na dawa ile. Baada ya hapo akaingia katika hali ya usingizi mzito wa kifo. Yule
mwungwana aliyekwisha kutajwa tayari akamwangalia mgonjwa yule na kusema kwa
masikitiko: "Siku zake zimekwisha. Juhudi zilizofanywa na mwili wake zimeshindwa mara
nyingi sana na sumu hii, hata nguvu zake za akiba zimekwisha kwa kutumika tena na tena
kufanya kazi hiyo isiyokuwa ya kawaida katika kuiondoa dawa hii yenye sumu kutoka
mwilini mwake. Nguvu zake za mwili sasa karibu zitakoma, na hapo ndipo maisha haya ya
mateso ya mgonjwa huyu yatakapokoma."

Vifo vingi vimesababishwa na kunywa madawa yenye sumu kuliko kwa sababu zote
nyingine zikijumlishwa pamoja. Kama katika nchi hii angekuwako mganga mmoja badala
ya maelfu waliopo, basi, vifo vingi sana vya watu wanaokufa kabla ya wakati wao
vingezuiwa. Makundi na makundi ya waganga, na madawa yao yenye sumu mengi mengi,
yameleta mateso kwa wakazi wa dunia hii, na kuwapeleka mapema kaburini maelfu na
makumi elfu.

Kujiendekeza kula mara kwa mara, na kula chakula kingi mno, huvilemea viungo vya
kuyeyusha chakula, na kuleta homa mwilini. Damu huwa chafu, na hapo ndipo magonjwa
ya kila aina hutokea. Mganga anaitwa, ambaye anaagiza dawa fulani yenye sumu inywewe,
ambayo inaleta nafuu kwa wakati huu tu, bali haiponyi ugonjwa huo. Inaweza kubadili tu
hali ya ugonjwa huo, lakini baa halisi huongezeka mara kumi zaidi. Mwili ulikuwa ukifanya
kila uliloweza ili kuondoa mkusanyiko wa uchafu kutoka mwilini; na kama ungeachiwa
wenyewe [kufanya kazi yake], ukisaidiwa na mibaraka ya kawaida kutoka mbinguni, kama
vile hewa safi, maji safi, basi, uponyaji wa haraka na ulio salama ungekuwa umefanyika.
Katika hali kama hizo wale wanaoteseka wanaweza kujifanyia wenyewe kile ambacho
wengine hawawezi kuwafanyia vizuri kama wao wenyewe wawezavyo. Wangeanza kwa
kuuondolea mwili mzigo ule mzito walioulazimisha juu yake. Wangepaswa kuiondoa
sababu ya ugonjwa huo kwa kufunga kwa kipindi kifupi, na kulipatia tumbo wasaa wa
kupumzika. Hali ile ya homa iliyomo mwilini ingepunguzwa kwa kutumia maji kwa
uangalifu na akili. Juhudi hizi zitausaudia mwili katika mapambano yake ya kuondoa
uchafu wote mwilini.

Lakini kwa kawaida watu wale wanaoteseka kwa maumivu huwa
hawana uvumilivu. Hawako tayari kujizoeza kujinyima chakula, na kuteseka kidogo kwa
njaa, wala hawako tayari kuingojea njia ile ya pole pole ya mwili ili upate kuzijenga upya
nguvu zake zilizopotea kutoka mwilini; bali wao wameamua kujipatia nafuu ya papo hapo,
na kwa ajili hiyo wanakunywa madawa ya sumu yenye nguvu, yaliyoamriwa na waganga
wao. Mwili ulikuwa unafanya kazi yake vizuri, nao ungeweza kupata ushindi; lakini wakati
unataka kuitimiza kazi yake, kitu kigeni cha aina ya sumu kikaingizwa mwilini. Ni kosa
lililoje! Mwili huo uliotendewa vibaya sasa unayo mabaa mawili kupigana nayo badala ya
lile moja. Unaiacha kazi ile uliyokuwa unaifanya, na kwa uthabiti unafanya juhudi
kumwondolea mbali mgeni huyo asiyetakiwa ambaye ameingizwa mwilini mwake hivi
karibuni [yaani, dawa ile yenye sumu]. Mwili unajisikia ya kwamba nguvu zake zinachotwa
maradufu kutoka katika akiba yake, nao unadhoofika.

Madawa yenye sumu kamwe hayaponyi ugonjwa. Yanabadilisha hali yake tu na mahali
pake ulipokuwapo. Mwili peke yake ndio unaorejesha afya kikamilifu, tena inakuwa vizuri
zaidi jinsi gani kwa mwili kuweza kuifanya kazi yake kama umeachwa wenyewe kufanya
hivyo! Lakini ruhusa hii kwa shida mno unapewa. Kama mwili uliolemewa unastahimili
chini ya mzigo huo, na hatimaye kwa kiwango fulani unafanikiwa kufanya kazi yake hiyo
ya maradufu, na mgonjwa huyo akaishi, basi, sifa anapewa mganga yule. Lakini mwili
ushindwapo katika juhudi yake ya kuiondoa sumu mwilini, na mgonjwa huyo akafa, basi,
tendo hilo huitwa amri ya ajabu ya maongozi yake Mungu. Kama mgonjwa huyo
angalikuwa amechukua njia ya kuupunguzia mwili wake mzigo huo mzito kwa wakati
wake, na kwa akili kutumia maji safi, basi, matumizi haya ya madawa yenye sumu
yanayoleta kifo yangeweza kuepukwa kabisa. Matumizi ya maji hayawezi kufanikiwa sana
kama mgonjwa huyo hatambui umuhimu wa kuangalia kwa makini sana maakuli yake.
Wengi wanaishi kwa kuzikiuka sheria za afya, nao wamekuwa wajinga wa kutojua
uhusiano uliopo kati ya mazoea yao ya kula, kunywa, na kufanya kazi, pamoja na afya yao.
Hawatagutuka kujua hali yao halisi mpaka hapo mwili wao utakapoanza kulalamika
kutokana na mateso unayopata kwa kutumiwa vibaya, kwa kusikia maumivu na uchungu
mwilini. Endapo, hata wakati huo, hao wanaoteseka wangeanza tu kufanya kazi ipasavyo,
na kutumia njia rahisi wanazozidharau, ----- matumizi ya maji na chakula kinachofaa, -----
mwili wao ungepata msaada ule unaouhitaji, na ambao ungekuwa umepewa muda mrefu
kabla yake. Endapo njia hii itafuatwa, basi, mgonjwa huyo kwa kawaida atapona bila kuwa
na udhaifu wo wote wa mwili.

Madawa hayo yenye sumu yanapoingia mwilini yanaweza kuonekana kwa wakati fulani
kuwa yanaleta manufaa mwilini. Badiliko linaweza kutokea mwilini, lakini ugonjwa
wenyewe usitibiwe. Utajidhihirisha wenyewe katika hali fulani nyingine. Mwili unapofanya
juhudi yake kuiondoa dawa hiyo yenye sumu kutoka mwilini, mateso makali mara nyingine
yanaweza kumpata mgonjwa huyo. Ugonjwa ambao dawa hiyo ilipewa kuutibu unaweza
kutoweka, lakini hatimaye unaweza kuonekana tena katika hali mpya, kama vile magonjwa
ya ngozi, vidonda, viungo vya mwili kuuma sana, na wakati mwingine katika hali ya hatari
zaidi na ya kufisha. Ini, moyo, na ubongo mara kwa mara huathirika kwa madawa haya
yenye sumu, na mara nyingi viungo hivi vinalemewa na ugonjwa; na watu hao wasio na
bahati endapo wataendelea kuwa hai, basi, watakuwa wagonjwa maisha yao yote,
wakijikongoja kwa uchovu na kuwa na maisha ya kusikitisha.

Ni gharama ilioje
iliyosababishwa na madawa hayo yenye sumu! Kama hayakugharimu uhai wa mtu, basi,
yaligharimu kiasi kikubwa mno. Pamoja na juhudi zake, mwili umeharibika. Mashine nzima
ya mwili wa mwanadamu imeharibika, na katika maisha yake ya baadaye, sehemu zile
zilizoharibika zitakapotumainiwa kufanya kazi yake muhimu zaidi kwa kushirikiana na
sehemu nyingine za mashine hii ya mwili, hazitaweza kuwa tayari kufanya kazi yake kwa
nguvu, na mwili wote utausikia upungufu huo. Viungo hivi, ambavyo vingekuwa katika hali
njema ya afya, vinadhoofika, na damu huwa chafu. Mwili utaendelea kupambana, na
mgonjwa huyo huugua magonjwa mengine yaliyo tofauti, mpaka mwili wote huvunjika
ghafula, na kifo kinafuata. Wengi hufa kutokana na matumizi ya madawa haya yenye sumu
kuliko kwa ugonjwa, kama mwili wao ungeachwa kufanya kazi yake wenyewe.

Watu wengi sana wamepoteza maisha yao kutokana na waganga kuwapa madawa yenye
sumu kwa magonjwa yasiyojulikana. Hawana ujuzi wo wote wa hakika kuhusu ugonjwa
halisi ulivyo unaomtesa mgonjwa huyo. Lakini waganga wanatazamiwa na watu kujua
upesi la kufanya; nao wasipofanya kazi yao upesi kana kwamba walikuwa wanaujua kabisa
ugonjwa huo, wanafikiriwa na marafiki zao wasiokuwa na subira, pamoja na wagonjwa
wenyewe, kuwa hawafai kabisa. Kwa hiyo, kuwaridhisha mawazo yao wagonjwa wale
pamoja na rafiki zao, ni lazima dawa itolewe, majaribio na vipimo vijaribiwe, ili kumtibu
mgonjwa ugonjwa wake ambao mganga huyo haujui kwa hakika. Mwili unajazwa na
madawa yenye sumu, ambayo unashindwa kuyatoa kutoka mwilini. Mara nyingi waganga
wenyewe wanaamini kwamba kifo kilitokana na matumizi yao ya madawa yenye nguvu
kwa ugonjwa ambao haukuwapo.

Waganga wanastahili kulaumiwa, lakini sio wao peke yao walio na makosa. Wagonjwa
wenyewe kama wangekuwa na subira, wangefunga kula chakula kwa muda fulani, na kwa
njia hiyo kuteseka kidogo, na kuupa mwili muda wa kupata nguvu tena, wangepona upesi
sana pasipo kutumia dawa yo yote. Mwili peke yake unazo nguvu za uponyaji. Madawa
hayana uwezo wo wote wa kuponya, lakini kwa kawaida, huuzuia mwili katika juhudi zake.
Hata hivyo, huo ndio unaolazimika kufanya kazi ile ya kuirejesha afya ya mwili. Wagonjwa
wana haraka kutaka kupona, na rafiki zao wamekosa subira. Ni lazima wapate dawa; nao
wasipoisikia nguvu ya dawa mwilini mwao kama mawazo yao potofu yanavyowaelekeza
kufikiri, basi, bila kuwa na subira wanamwita mganga mwingine. Mabadiliko hayo mara
nyingi huzidisha baa hilo. Wanapewa dawa zenye hatari kama zile za kwanza, na za kufisha
zaidi, kwa kuwa matibabu hayo mawili hayapatani, na mwili unasumishwa kupita upeo
wake wa kuponywa.

Walakini wengi hawajaona kamwe manufaa ya matumizi ya maji, nao wanaogopa kutumia
mmojawapo wa mibaraka mikuu kuliko yote itokayo Mbinguni. Watu wale wanaoteseka na
homa zenye joto kali sana wananyimwa maji kwa kuogopa kwamba yatawadhuru. Endapo
katika hali yao ya homa kali, wangepewa maji mengi ya kunywa, na matumizi ya maji pia
yangefanyika nje ya mwili wao, siku ndefu na usiku mrefu wa mateso vingefupizwa, na
maisha ya thamani ya watu wengi yangeachiliwa. Hata hivyo maelfu wamekufa wakiwa na
homa kali sana zikiwatesa mpaka moto ulioichochea homa hiyo umemalizika, na viungo
muhimu kuteketea; wamekufa wakiwa na maumivu machungu mno, pasipo kuruhusiwa
kupewa maji ya kutuliza kiu yao inayowaka kama moto. Maji, ambayo yanatumika kuzima
moto wa jengo lisilokuwa na akili, hayaruhusiwi kuwapa wanadamu kuzima moto
unaoteketeza viungo vyao muhimu.

Makundi kwa makundi wanabaki na ujinga wao usiosameheka kuhusu sheria zile
zinazotawala maumbile yao. Wanashangaa kwa nini wanadamu wamekuwa dhaifu mno, na
kwa nini wengi hufa mapema kabla ya wakati wao. Je, hakuna sababu yake? Waganga,
wanaojidai kuujua mwili wa mwanadamu, wanatoa kwa wagonjwa wao, na hata kwa watoto
wao wenyewe wanaowapenda, pamoja na wenzi wao, dawa hizi zenye sumu inayofanya
kazi yake pole pole mwilini ili kuuondoa ugonjwa huo, au kutibu hali fulani ya ugonjwa
mtu asipojisikia vizuri. Kwa kweli hawawezi kutambua ubaya wa vitu hivyo, la sivyo,
wasingefanya hivyo. Matokeo yanayoletwa na sumu hizo huenda yasionekane mara moja,
lakini sumu hiyo inaendelea kufanya kazi yake mwilini, ikiharibu afya ya mwili, na
kuufanya mwili ushindwe katika juhudi zake za mapambano. Wanajaribu kusahihisha baa
moja, lakini wanazalisha baa kubwa zaidi ambalo mara nyingi haliponyeki.

Wale
wanaoshughulikiwa hivyo, daima wanakuwa wagonjwa, nao wanaendelea daima kunywa
madawa hayo yenye sumu. Lakini, kama utayasikiliza maongezi yao, siku zote utawasikia
wakiyasifu madawa hayo yenye sumu ambayo wamekuwa wakiyatumia, nao
wanapendekeza kwa wengine kuyatumia, kwa sababu, kama wasemavyo, wamefaidika kwa
kuyatumia.. Ingeonekana ya kwamba kwa wale wanaofikiri kwa kuchunguza sababu na
matokeo yake, wangepata ushahidi wa kutosha wa madawa hayo yenye sumu
yanavyoharibu afya, kwa kuangalia nyuso zilizogeuka rangi na kuwa manjano nyeupe,
pamoja na malalamiko ya kudumu ya magonjwa mbalimbali, na unyong'onyevu wa jumla
kutoka kwa wale wanaodai kunufaika nayo. Lakini wengi wamepofuka macho hata hawaoni
kwamba madawa yote yenye sumu waliyokunywa hayajaweza kuwaponya, bali
yamewafanya wajisikie vibaya zaidi. Mgonjwa yule anayetumia madawa yenye sumu
anachukua nafasi ya kwanza duniani, lakini kwa kawaida yeye ni mwepesi wa kukasirika,
anayo harara, siku zote yeye ni mgonjwa tu, anaishi kwa kujikongoja maisha ya kusikitisha,
naye anaonekana kuishi kwa kuhitaji siku zote kwamba wengine ndio wajizoeze kuwa na
subira kwake. Madawa hayo yenye sumu hayajamwua mara moja, maana mwili unachukia
kuuachilia uhai wake; hauko tayari kuacha mapambano yake. Walakini wale wanaotumia
madawa hayo yenye sumu hawawezi kuwa wazima.

Aina mbalimbali zisizokwisha za madawa zinauzwa katika soko la madawa, matangazo
mengi ya madawa mapya na michanganyo mipya, ambayo, wao wanasema, huleta matokeo
mazuri ya uponyaji wa ajabu, huwa yanawaua mamia mahali ambapo mmoja tu ananufaika.
Wale ambao ni wagonjwa huwa hawana subira. Watakunywa madawa hayo mbalimbali,
mengine ambayo yana nguvu nyingi sana, japokuwa hawayajui madawa hayo
yalivyochanganywa. Madawa yote wanayokunywa hufanya tu kupona kwao kusiwe na
matumaini yo yote. Hata hivyo, wao wanaendelea tu kuyanywa, nao wanazidi kuwa na hali
mbaya zaidi mpaka wanapokufa. Wengine wanataka wapewe dawa kwa vyo vyote vile.
Haya! na wajichukulie jukumu la kunywa michanganyo hiyo ya madawa yanayodhuru
mwili, pamoja na kunywa sumu za kufisha mbalimbali. Watumishi wa Mungu
wasingepaswa kutoa madawa, ambayo wanajua yataacha nyuma yake matokeo yanayoleta
madhara mwilini, hata kama watawapatia nafuu wagonjwa wao kutokana na maumivu ya
sasa.

Itaendelea....