Mtayarishaji

Morning Star Radio

Jumatano, Novemba 26, 2014

Mdomo wa Ndege aitwaye Mdiria

Kule Japani, treni inayosafiri mwendo wa kilomita 300 kwa saa ndiyo yenye mwendo wa kasi zaidi ulimwenguni. Kwa kiasi fulani, mdiria ambaye ni ndege mdogo sana, amechangia sana kufanikiwa kwa treni hiyo. Jinsi gani?

 

Fikiria hili: Mdiria anaweza kuzama ndani ya maji bila kuyafanya yaruke sana anapotafuta chakula. Jambo hilo lilimvutia sana Eiji Nakatsu, injinia aliyesimamia majaribio ya treni hiyo. Alijiuliza jinsi mdiria anavyoweza kustahimili badiliko hilo kutoka hewani kuingia majini. Jibu la swali hilo lingetatua tatizo kubwa lililokuwa likiikumba treni hiyo inayosafiri kwa kasi. Nakatsu anaeleza hivi: “Treni inapoingia chini ya ardhi kwa kasi sana inatokeza mawimbi ya shinikizo la hewa ambayo huongezeka zaidi na zaidi. Mawimbi hayo hufika mwisho wa barabara hiyo ya chini ya ardhi kwa kasi ya mwendo wa sauti na hivyo kutokeza sauti kama ya mlipuko na tetemeko kubwa hivi kwamba wakazi wanaoishi umbali wa mita 400 walilalamika.”

  
Uamuzi ulifanywa ili kuunda treni hiyo kwa umbo la mdomo wa mdiria. Kulikuwa na matokeo gani? Sasa treni hiyo inasonga kasi zaidi kwa asilimia 10 na kutumia nguvu kidogo zaidi kwa asilimia 15. Zaidi ya hilo, shinikizo la hewa linalotokezwa na treni hiyo limepungua kwa asilimia 30. Kwa sababu hiyo, hakuna sauti ya mlipuko treni hiyo inapopita katika barabara hiyo ya chini ya ardhi.


Una maoni gani? Je, mdomo wa mdiria ulijitokeza wenyewe? Au ulibuniwa?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni