Mtayarishaji

Morning Star Radio

Jumapili, Machi 02, 2014

Muziki ni wa maana kwako kadiri gani?


□ Si wa lazima.
□ Siwezi kuishi bila muziki.

Wewe husikiliza muziki wakati gani?

□ Ninaposafiri
□ Ninaposoma
□ Wakati wote

Ni muziki wa aina gani unaopenda sana?

YAELEKEA sote tuliumbwa tukiwa na uwezo wa kufurahia muziki. Na kwa vijana wengi, muziki ni wa lazima. “Siwezi kuishi bila muziki,” anasema Amber mwenye umri wa miaka 21. “Mimi husikiliza muziki karibu kila wakati, ninapofanya usafi, ninapopika, ninapotembea, au hata ninaposoma.”

Hata muziki wenye mdundo wa kawaida tu unaweza kupenya ndani sana na kuchochea hisia zetu. Kama vile “neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” wimbo unaochezwa wakati unaofaa unaweza kuburudisha sana! (Methali 15:23) “Nyakati nyingine unahisi kwamba hakuna mtu anayekuelewa,” anasema Jessica mwenye umri wa miaka 16. “Lakini ninaposikiliza nyimbo za bendi fulani ninayopenda, najihisi kwamba siko peke yangu.”

Je, Muziki Hutokeza Vita au Amani?

Ingawa unapenda muziki, huenda wazazi wako wakawa na maoni tofauti. Kijana mmoja anasema: “Baba yangu husema, ‘Zima hiyo kilele! Inaniumiza masikio!’” Ugomvi unapotokea, huenda ukaona kwamba wazazi wako wanachemka bure. “Ilikuwaje walipokuwa vijana?” anauliza msichana mmoja. “Kwani wazazi wao pia hawakufikiri kwamba muziki walioupenda ulikuwa mbaya?” Ingred mwenye umri wa miaka 16 analalamika: “Watu wazima hawapendi mabadiliko. Ingekuwa afadhali kama wangetambua kwamba kizazi chetu kinapenda muziki tofauti!”

Kuna ukweli fulani katika maneno ya Ingred. Kama ujuavyo, tangu zamani mapendezi ya vijana na ya watu wazima yametofautiana sana. Hata hivyo, haimaanishi kwamba lazima mgombane kwa sababu ya muziki kila siku. Siri ni kujaribu kutafuta maelewano kuhusu muziki. Ikiwa wazazi wako wanaiheshimu Biblia, basi kuna matumaini. Kwa nini? Kwa kuwa Neno la Mungu linaweza kukusaidia wewe na wazazi wako kutambua mambo yanayofaa na yanayotegemea mapendezi ya kibinafsi. Ili kufanya hivyo, unahitaji kuchanganua mambo mawili makuu: (1) ujumbe ulio katika muziki unaosikiliza na (2) muda unaotumia kusikiliza muziki. Kwanza, tufikirie swali hili . . .

Muziki Ninaopenda Una Ujumbe Gani?

Muziki ni kama chakula. Unahitaji aina inayofaa kwa kiasi kinachofaa. Aina mbaya, hata iwe ni kiasi gani, ni hatari. Kwa kusikitisha, katika ulimwengu wa muziki, aina mbaya ya muziki ndiyo inayovutia zaidi. “Kwa nini miziki yote yenye midundo mitamu huwa na maneno machafu hivyo?” alalamika kijana anayeitwa Steve.

Ikiwa unapendezwa na mdundo, kuna haja ya kuzingatia ujumbe uliopo? Ili kujibu swali hilo, jiulize: ‘Ikiwa mtu fulani angetaka ninywe sumu, angetumia mbinu gani ili kunifanya niinywe? Je, angeichovya katika kitu kichungu au katika sukari?’ Yule mwanamume mwaminifu, Ayubu, aliuliza: “Je, sikio halipimi maneno kama kaakaa linavyoonja chakula?” (Ayubu 12:11) Kwa hiyo, badala ya kusikiliza muziki kwa sababu tu unapenda mdundo wake—utamu wake wa kijuujuu—‘pima maneno yake’ kwa kufikiria kichwa cha muziki na maneno yaliyomo. Kwa nini? Kwa sababu maneno yaliyo katika muziki yataathiri kufikiri kwako na mtazamo wako.

Inasikitisha kwamba miziki inayopendwa sana leo ina maneno yanayosifu ngono, jeuri, na matumizi ya dawa za kulevya. Ikiwa huoni kwamba kusikiliza maneno hayo kunaweza kukuathiri, basi “sumu” yake imeanza kukuingia.

Usifuate Upepo

Vijana wenzako wanaweza kukushinikiza usikilize muziki usiofaa. Pia, soko la muziki lina uvutano mkubwa. Kukiwa na redio, Intaneti, na televisheni, muziki umekuwa biashara kubwa. Wataalamu wa mauzo wameajiriwa ili kukuchochea upendezwe na muziki wa aina fulani.

Lakini unapoacha marafiki au vyombo vya habari vikuamulie muziki utakaosikiliza, unapoteza uhuru wako wa kuchagua. Unakuwa mtumwa, mtu asiyetumia akili yake. (Waroma 6:16) Biblia inakuhimiza uepuke uvutano wa ulimwengu katika mambo kama hayo. (Waroma 12:2) Hivyo, unapaswa kuzoeza ‘nguvu zako za ufahamu ili zitofautishe yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Unaweza kutumia jinsi gani nguvu zako za ufahamu unapochagua muziki? Fikiria mapendekezo yanayofuata:

Chunguza picha na maandishi yaliyo kwenye kasha. Mara nyingi unaweza kujua yaliyomo katika kanda kwa kutazama kasha. Unapoona picha zinazoonyesha jeuri, ngono, au kuwasiliana na pepo, tahadhari. Inaelekea muziki wenyewe pia haufai.

Soma maneno ya wimbo. Ni nini kinachosemwa? Je, kweli ungependa kusikiliza maneno hayo tena na tena? Je, ujumbe wa wimbo huo unapatana na sifa na kanuni za Kikristo?—Waefeso 5:3-5.

Chunguza athari zake. Kijana anayeitwa Philip anasema: “Niligundua kwamba muziki na maneno niliyosikiliza yalinifanya nishuke moyo.” Kwa kweli, muziki unaweza kuathiri watu kwa njia mbalimbali. Lakini muziki unaosikiliza unaamsha hisia gani? Jiulize: ‘Je, mimi huwa na mawazo yasiyofaa baada ya kusikiliza muziki au maneno ya muziki fulani? Je, nimeanza kutumia lugha ya mitaani inayotumiwa katika muziki?’—1 Wakorintho 15:33.

Wafikirie wengine. Wazazi wako wana maoni gani kuhusu muziki unaosikiliza? Waulize maoni yao. Pia, fikiria maoni ya Wakristo wenzako. Je, wengine wanaweza kukwazwa? Kubadili mwenendo wako ili usiumize hisia za wengine kunaonyesha kwamba wewe ni mkomavu.—Waroma 15:1, 2.

Kujiuliza maswali yaliyo hapo juu kutakusaidia kuchagua muziki ambao utakuchangamsha moyo pasipo kuangamiza hali yako ya kiroho. Hata hivyo, kuna jambo lingine la kufikiria.

Ni Wakati Gani Muziki Unapita Kiasi?

Muziki unaofaa kama vile chakula kizuri unaweza kuwa wenye faida. Hata hivyo, methali yenye hekima inaonya: “Je, umepata asali? Kula kiasi cha kukutosha, ili usiile kupita kiasi kisha uitapike.” (Methali 25:16) Asali ni dawa. Lakini kitu chochote hata kiwe kizuri kinapopita kiasi kinaweza kukudhuru. Kwa hiyo, vitu vizuri vinapaswa kufurahiwa kwa kiasi.

Hata hivyo, maisha ya vijana fulani hutawaliwa na muziki. Kwa mfano, Jessica aliyetajwa mapema, anakiri: “Mimi husikiliza muziki kila wakati—hata ninapojifunza Biblia. Mimi huwaambia wazazi wangu kwamba muziki hunisaidia kukaza fikira. Lakini hawaniamini.” Je, umewahi kuwa na maoni kama ya Jessica?
Unaweza kujua jinsi gani ikiwa unapita kiasi katika kusikiliza muziki? Jiulize maswali yanayofuata:

Kila siku mimi hutumia saa ngapi kusikiliza muziki? ․․․․․
Ninatumia pesa ngapi kwa muziki kila mwezi? ․․․․․

Je, muziki unaharibu uhusiano kati yangu na wengine katika familia? Ikiwa ndivyo, andika hapa chini jinsi unavyoweza kurekebisha hali hiyo. ․․․․․

Badili Mazoea Yako

Ikiwa muziki unachukua wakati mwingi kupita kiasi, unapaswa kujiwekea mipaka na kuwa na usawaziko kuhusiana na mazoea yako ya kusikiliza muziki. Kwa mfano, huenda ukahitaji kuacha mazoea ya kuweka masikioni vidude vya kusikilizia muziki siku nzima au mazoea ya kuwasha redio mara tu unapofika nyumbani.
Kwa nini usijifunze kufurahia pindi za utulivu, pasipo kelele yoyote? Kufanya hivyo kutakusaidia katika masomo yako. 

Steve aliyetajwa mapema anasema: “Unaweza kujifunza mambo mengi zaidi ikiwa muziki umezimwa.” Jaribu kusoma bila muziki, na uone iwapo utakazia fikira zaidi mambo unayojifunza.
Pia, utahitaji kupanga wakati wa kusoma na kujifunza Biblia na vitabu vinavyotegemea Biblia. Nyakati nyingine, Yesu Kristo alitafuta mahali patulivu ili kusali na kutafakari. (Marko 1:35) Je, wewe pia hujifunza katika mazingira matulivu, yasiyo na kelele? Ikiwa hufanyi hivyo, huenda unazuia ukuzi wako wa kiroho.

Fanya Uchaguzi Unaofaa

Kwa kweli, muziki ni zawadi kutoka kwa Mungu, lakini unapaswa kujihadhari usiitumie vibaya. Usiwe kama msichana anayeitwa Marlene, anayesema: “Nina muziki ambao ninajua ninapaswa kuutupilia mbali. Lakini ni mtamu wee.” Fikiria madhara anayosababisha katika akili na moyo wake kwa kusikiliza muziki usiofaa! Usinaswe na mtego huo. Usikubali muziki ukupotoshe au utawale maisha yako. Chagua muziki unaopatana na viwango vya Kikristo. Mwombe Mungu akusaidie. Tafuta marafiki walio na maoni kama yako.

Muziki unaweza kukustarehesha na kukuburudisha. Unaweza kukuondolea hisia za upweke. Hata hivyo, hautatui matatizo yako. Isitoshe, nyimbo haziwezi kulinganishwa na marafiki wa kweli. Kwa hiyo, usiruhusu muziki uwe jambo kuu maishani mwako. Furahia muziki, lakini usikubali ukutawale.


Unahitaji kujiburudisha mara kwa mara. Kanuni za Biblia zinaweza kukusaidia jinsi gani unufaike kutokana na pindi hizo zenye kufurahisha?

MAANDIKO MUHIMU

Je, sikio halipimi maneno kama kaakaa linavyoonja chakula?Ayubu 12:11.

PENDEKEZO

Ikiwa unataka wazazi wako waelewe ni kwa nini unapenda muziki au bendi fulani, kwanza jaribu kupendezwa na baadhi ya miziki wanayofurahia.

JE, WAJUA . . .?

Ikiwa hupendi wazazi wako wasikilize muziki unaopenda sana, basi huenda muziki unaosikiliza una kasoro.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ninaweza kuwa na usawaziko kuelekea muziki niki ․․․․․
Vijana wenzangu wakinishurutisha nisikilize muziki usiofaa, nitawaambia ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

Kwa nini uchaguzi wako wa muziki ni wa maana sana?
Unaweza kuamua jinsi gani ikiwa wimbo fulani unafaa au haufai?
Unaweza kufanya nini ili ujifunze kufurahia miziki ya aina nyingine?

‘‘Wakati mwingine mimi hujikuta nikisikiliza muziki usiofaa. Nauzima bila kukawia. Nisipofanya hivyo mara moja, nitaanza kutafuta visababu vya kuusikiliza.’’—Cameron

Jifunze Kufurahia Miziki ya Aina Nyingine

  Je, unapenda aina nyingi zaidi za chakula leo kuliko ulipokuwa na umri wa miaka mitano? Ikiwa ndivyo, ni kwa sababu umejizoeza kufurahia ladha ya vyakula vipya. Ndivyo ilivyo na muziki. Usisikilize muziki wa aina moja tu. Jifunze kupendezwa na miziki ya aina nyingine.

  Njia moja ya kufanya hivyo ni kujifunza kupiga ala fulani ya muziki. Kufanya hivyo kunaweza kukuchangamsha na kukuridhisha na pia kutakufanya upendezwe na aina nyingine ya muziki mbali na ile inayopigiwa debe na wafanyabiashara. Utapata wapi wakati wa kujifunza? Unaweza kupunguza wakati unaotumia kutazama televisheni au kucheza michezo ya kompyuta. Ona yale ambayo vijana hawa wanasema.

“Kupiga ala ya muziki ni raha na kunaweza kuwa njia bora ya kuonyesha hisia zako. Kujifunza kupiga nyimbo mpya kumenisaidia kupenda aina mbalimbali za muziki.”—Brian, mwenye umri wa 18, ambaye hupiga gitaa, ngoma, na piano.

“Unahitaji kufanya mazoezi ikiwa unataka kujifunza kupiga vizuri chombo fulani cha muziki. Na mazoezi hayafurahishi sikuzote. Lakini kuwa stadi wa kupiga muziki fulani ni jambo lenye kufurahisha na kuridhisha kwelikweli.”—Jade, mwenye umri wa miaka 13, ambaye hupiga fidla.

“Ninapokuwa nimechoka au kushuka moyo, kupiga gitaa hunisaidia kustarehe. Kutunga muziki mzuri na wenye kutuliza na kuburudisha ni jambo lisilo na kifani.”—Vanessa, mwenye umri wa miaka 20, hupiga gitaa, piano, na zumari.

“Nilikuwa nikijiambia, ‘Sitawahi kuwa na ustadi kama fulani wa fulani.’ Lakini niliendelea kufanya mazoezi, na sasa ninapata uradhi ninapopiga wimbo fulani vizuri. Sasa, nawavulia kofia wanamuziki wengine stadi.”—Jacob, mwenye umri wa miaka 20, hupiga gitaa.

Muziki ni kama chakula. Unahitaji aina inayofaa kwa kiasi kinachofaa. Aina mbaya, hata iwe ni kiasi gani, ni hatari

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni