Mtayarishaji

Morning Star Radio

Ijumaa, Desemba 05, 2014

Nyigu na Mrija Utoboao Miti






 Nyigu wa kike ambaye hutoboa miti na kutaga mayai ndani ya misonabari, amewashangaza sana wanasayansi kwa mbinu yake ya kutoboa miti na kuwachochea kubuni vifaa bora zaidi vya kufanya upasuaji kwa njia salama zaidi.

Fikiria hili: 

Nyigu huyo hutoboa msonobari kwa kutumia mrija ulio kama sindano na wenye mitaimbo miwili, au “valvu” zilizoingiana, ambapo kila moja imefunikwa kwa meno yanayoangalia nyuma. Meno ya valvu moja hushikilia mti na hivyo kumfanya asisonge, na valvu ile nyingine husonga hatua moja mbele. 

Kisha meno ya valvu hiyo ya pili hushikilia mti tena na hivyo ile valvu ya kwanza inasonga mbele. Katika mwendo huu wa kasi unaofanyika kwa kurudia-rudia—ambapo valvu hizo hubadilishana kushikilia mti na kusonga mbele—mrija huo huchimba milimita 20 hivi bila kutumia nguvu nyingi kwenye sehemu laini ya nje ya mti bila kujipinda wala kuvunjika.


Wanasayansi wamechochewa na mrija huo hivi kwamba wanabuni kifaa cha kufanya upasuaji katika ubongo ambacho kitachimba kwa kutumia mbinu hiyo. Sindano yake ya silikoni ina valvu mbili ambazo husonga mbele na nyuma, kila moja ikiwa na meno madogo ambayo yanaweza kuingia katika sehemu za ndani zaidi za ubongo bila kusababisha madhara makubwa. Hata hivyo, kifaa hicho kitaweza kufanya jambo lingine. 

Gazeti New Scientist linaeleza, “Tofauti na vifaa vingine vya upasuaji visivyoweza kujipinda, kifaa hiki kitaweza kujipinda kwa kiasi kikubwa hivi kwamba kitapitishwa katika sehemu salama zaidi za ubongo, bila kugusa sehemu nyeti wakati wa upasuaji.” Kifaa hicho pia kitafanya iwe rahisi kufikia sehemu ambazo huwa ni vigumu kufikia bila kukata viungo ambavyo havina tatizo.

Zaidi INGIA HAPA

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni